Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Aprili 19, 2024 Local time: 10:51

Polisi wamkamata Bobi Wine alipowasili Kampala


Wakazi waamrisha kutoka nje ya majumba yao wakati vyombo vya usalama vikiwafuatilia waandamanaji mjini Kampala, Uganda, Agosti 20, 2018.
Wakazi waamrisha kutoka nje ya majumba yao wakati vyombo vya usalama vikiwafuatilia waandamanaji mjini Kampala, Uganda, Agosti 20, 2018.

Mbunge wa upinzani nchini Uganda na mwanamuziki wa kizazi kipya Bobi Wine amepokewa na polisi Alhamisi mchana alipowasili uwanja wa ndege mjini Kampala, na kuwekwa kizuizini.

Waandishi wa habari hawakuruhusiwa kufika uwanja wa ndege na ulinzi umeimarishwa kote mjini Kampala, wakati vikosi vya usalama vimepelekwa mitaani na vinadhibiti njia zote zinazoelekea uwanja wa ndege. Siku ya Jumatano, polisi walipiga marufuku watu kukusanyika uwanja wa ndege au sehemu nyingine kumlaki Wine mwenye umri wa miaka 36.

Vyombo vya habari vya kimataifa na ndani ya nchi, pamoja na ripoti za mitandao ya jamii zinaeleza kuwa kaka yake Wine, wanamuziki wa bendi yake na meneja wake walikamatwa muda mfupi kabla ya kuwasili wake akitokea Ulaya.

Wine, ambaye jina lake halisi ni Robert Kyagulanyi alikuwa Marekani kwa kipindi cha wiki chache, akifuatilia matibabu ya majiraha aliyopata ambayo amesema yametokana na vipigo alivyopata baada ya kukamatwa Agosti 14.

Kwa muda mrefu amekuwa mkosoaji wa Rais Yoweri Museveni, ambaye amekuwepo madarakani kwa zaidi ya miaka 30. Wine, wabunge wengine wanne na kiasi cha wafuasi wake 30 walikamatwa mwezi uliopita baada ya maandamano kufanyika wakati wa shughuli za kampeni za uchaguzi mdogo.

Wine amesema kuwa yeye pamoja na wenziwe waliteswa wakiwa kizuizini. Alipewa dhamana na kuruhusiwa kuondoka nchini kwende kujitibia. Serikali imekanusha madai hayo ya kuteswa kwake na kunyanyaswa.

Museveni, ambaye ana umri wa miaka 74, bado ni maarufu katika baadhi ya makundi ya Waganda, kwa kuleta utulivu nchini humo. Lakini, zaidi ya asilimia 70 ya wananchi wana umri wa chini ya miaka 35 na wengi wa wapiga kura katika kundi hili wanasema wanataka kiongozi kijana.

XS
SM
MD
LG