Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Machi 29, 2024 Local time: 17:27

May anusurika kuondolewa madarakani


Waziri Mkuu wa UIngereza Theresa May
Waziri Mkuu wa UIngereza Theresa May

Waziri Mkuu wa Uingereza Theresa May amenusurika kuondolewa katika wadhifa wake kupitia kura ya kutokuwa na imani naye iliyopigwa Jumatano, siku moja baada ya bunge kwa sauti moja kupiga kura dhidi ya mpango wake wa kuiondoa Uingereza kutoka Umoja wa Ulaya.

Kunusurika huko kuondolewa kutamwezesha May kuangalia njia ya kupata makubaliano ya Brexit kupitia bunge. Anafursa hadi Jumatatu kutoa pendekezo jipya katika bunge la makabwela, lakini haijulikani kitu gani atapendekeza.

Muda mfupi baada ya kupigwa kura 325 kwa 306 ambazo zilimwezesha May kubakia madarakani, alitoa mwaliko kwa viongozi wa chama hicho kushiriki katika mazungumzo ya Brexit Jumatano usiku.

May alisema kabla ya kupigwa kura hiyo Jumatano kuwa Uingereza itajiondoa kutoka Umoja wa Ulaya ifikapo Machi 29 tarehe iliyokuwa imekusudiwa, na umoja huo utafikiria tu kuongeza muda wa mazungumzo iwapo tu kuna mpango wa uhakika wa kujiondoa.

Wasaidizi wa waziri mkuu wamesema atajaribu kuvuta muda zaidi na kurejea Brussels kujaribu kuwashawishi viongozi wa EU kufanya mazungumzo tena.

Viongozi wa EU wameendelea kukataa kuwa kuna uwezekano wa mazungumzo kufanyika tena ilivyo kuwa kwamba makubaliano yalishafikiwa mwezi Novemba 2018.

Lakini maafisa wa Uingereza wanamatarajio kuwa Brussels hivi sasa inawezekana ikalegeza masharti ya kutosha kuwezesha mpango huo kuungwa mkono na bunge kwa ajili ya marudio ya kura katika marekebisho ya makubaliano hayo.

XS
SM
MD
LG