Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Julai 27, 2024 Local time: 05:02

Matokeo ya utafiti yamsukuma Trump kuhimiza uvaaji barakoa


Rais Donald Trump
Rais Donald Trump

Wachambuzi nchini Marekani wanasema Rais Donald Trump amelazimika kubadili msimamo wake kuwataka Wamarekani kuvaa barakoa baada ya kuonekana anashindwa katika utafiti wa maoni na mpinzani wake Joe Biden kwa ajili ya uchaguzi wa Novemba.

Wachambuzi nchini Marekani wanasema Rais Donald Trump amelazimika kubadili msimamo wake kuwataka Wamarekani kuvaa barakoa baada ya kuonekana anashindwa katika utafiti wa maoni na mpinzani wake Joe Biden kwa ajili ya uchaguzi wa Novemba.

Rais Donald Trump Jumanne akirudia tena mikutano ya kueleza juu ya hali ya virusi vya corona alionekana kubadili kabisa msimamo wake kuhusiana na namna ya kukabiliana na janga hili la Corona.

Kulingana na utafiti wa hivi karibuni kutoka kampuni ya kukusanya maoni ya Pew, ni wamarekani asilimia 65 pekee ambao huvaa barakoa wakati wakiwa kwenye maeneo ya umma kama vile madukani au kwenye biashara.

Baada ya miezi kadhaa ya kupuuzia umuhimu wa kuvaa barakoa, Trump mapema wiki hii kupitia ujumbe wa twitter amesema kuwa kuvaa barakoa kunaonyesha uzalendo wakati akiweka picha yake amevaa barakoa akihimiza umuhimu wa kuvaa barakoa.

Rais amesema : "Sasa hivi mimi ninayo maski yangu ambayo nina ibeba kila ninapokwenda na kuitumia bila shida. Nahimiza umuhimu wa kuvaa barakoa wakati ukikaribiana na mwenzako au ukiwa kwenye kundi la watu. Mimi nitaiva nikiwa katika kundi la watu.

Mwezi Aprili, kituo cha kitaifa cha kudhibiti magonjwa ya maambukizi hapa Marekani CDC, kilibatilisha msimamo wa awali na kusema kuwa sasa Wamarekani wote wanahitajika kuvaa barakoa na sio wahudumu wa afya pekee kama ilivyo kuwa imeelekeza muda mfupi baada ya janga kutokea.

Hata hivyo Rais Trump hakuwa akivalia akiwa mbele ya umma hadi mapema mwezi Julai. Alikuwa pia amekwepa kuhimiza umuhimu wa kutumia barakoa akisema anaheshimu uhuru wa watu kujiamulia mambo yao.

Uchunguzi wa maoni wa hivi karibuni ulofanywa na shirika la habari la ABC pamoja na gazeti la Washington Post unaonyesha kuwa asilimia 64 ya Wamarekani hawajaridhishwa na namna Trump aliovyochukulia janga hilo.

Norman Ornstein ni msomi kutoka taasisi ya American Enterprise na anasema kuwa msimamo wa Trump unaonekana kusababisha matatizo.

Ornstein anasema : "Msimamo huo unasababisha matatizo zaidi kwake yeye wakati janga likiendelea kuenea hata hivi sasa kwenye maeneo ambapo magavana wa Repablikan walifuata msimamo wake na kufungua tena shuguli za kawaida, na sasa matokeo yake ni ongezeko kubwa la kasi ya maambukizi, suala ambalo linafanya kazi yake kuwa ngumu zaidi.

Kufikia sasa, Marekani imeshuhudia zaidi ya watu milioni 3.8 walioambukizwa na COVID-19 , na vifo zaidi ya 140,000 wakati takwimu za hivi karibuni kutoka CDC zikionyesha kuwa idadi hiyo huenda ikawa kubwa maradufu.

Ingawa utawala unasema kuwa ongezeko la idadi ya maambuzi ni kutokana na kuongezwa kwa upimaji. Wataalam wanakosoa dhana hiyo kutokana na sera mbovu za kitaifa katika kukabiliana na janga hilo.

William Schaffner ni mtaalam wa majaga ya magonjwa kutoka chuo kikuu cha Vanderbilt anasema : "Mataifa yaliofaulu katika kudhibiti maambukizi yalikuwa na sera wazi za kitaifa zinazo zingatia afya ya watu wake. Viongozi wa kisiasa walishirikiana na wahudumu wa afya katika kueneza ujumbe wa kujiepusha na maambukizi. Watu walieleweshwa kuhusu umuhimu wa kujikinga na walifuata maagizo. Hiyo ilikuwa mbinu ilioleta ushindi mkubwa kinyume na magavana waliovyoachiwa kufanya maamuzi yao hapa Marekani."

Licha ya ongezeko kubwa la maambukizi, wamarekani wameendelea kufurika kwenye maeneo ya mapumziko mnamo kipindi hichi cha majira ya joto . Majimbo tofauti yana sheria tofauti kuhusiana na kujikinga na maambukizi wakati pendekezo la serikali kuu la kuvalia barakoa pamoja na kufunguliwa kwa uchumi likifanywa kwa hiari kwenye majimbo tofauti.

XS
SM
MD
LG