Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumapili, Mei 19, 2024 Local time: 03:49

Kimbunga Kenneth chapungua kasi Tanzania, chaelekea Msumbiji


Wafanyakazi wa Shirika la Misaada la Marekani (USAID) wakiendelea kuwasaidia wananchi nchini Msumbiji
Wafanyakazi wa Shirika la Misaada la Marekani (USAID) wakiendelea kuwasaidia wananchi nchini Msumbiji

Mamlaka ya hali ya hewa nchini Tanzania imesema kimbunga Kenneth hivi sasa kimebadilisha muelekeo na kuwa sio tishio tena kwa wananchi wa mikoa ya Lindi na Mtwara.

Taarifa ya Mamlaka ya Hali ya Hewa nchini Tanzania inaeleza hivi sasa kimbunga kinaendelea kusogea kaskazini mwa Msumbiji katika mji wa Cabo Delgado.

Mkuu wa Mkoa wa Mtwara Gelasius Byakanwa ameiambia Sauti ya Amerika (VOA) kuwa hivi sasa wananchi wamefahamishwa kuwa wanaweza kuendelea na maisha yao kama kawaida na kurudi majumbani kutokana na kimbunga Kenneth kubadilisha muelekeo.

Kennes Bwire : Mahojiano Maalum na Mkuu wa Mkoa wa Mtwara
please wait

No media source currently available

0:00 0:05:24 0:00

Utabiri wa hali ya hewa ulionyesha kuwa Kimbunga Kenneth kingetarajiwa kuingia nchi Kavu katika eneo la nchi ya Msumbiji umbali wa kilomita 237 kutoka eneo la Pwani ya Mtwara, siku ya Alhamisi usiku.

Mkuu wa Mkoa amesema idara ya hali ya hewa imetangaza kuwa kimbunga hicho kimepungua kasi na kufikia kilomita 50 nchini Tanzania kwa sasa.

Katika maeneo ya Mtwara wananchi walionekana kuchukua tahadhari hasa kwa kuelekea katika maeneo yaliyotengwa na serikali kwa ajili ya kujikinga dhidi ya Kimbunga Kenneth ikiwemo uwanja wa ndege wa Mtwara na maeneo ya shule ambayo ni salama.

Nayo Serikali kupitia Waziri mwenye dhamana ya kushughulikia majanga kama haya, Jenista Mhagama, ilitoa maelekezo ikizitaka mamlaka na Idara zote zikiwemo za uokozi kujipanga kikamilifu kukabiliana na athari za Kimbunga Kenneth pamoja na kuendelea kutoa tahadhari kwa wananchi.

Kimbunga Kenneth kitakua cha kwanza cha ukubwa huu kufika Tanzania, tangu mwaka 1952, nchi hiyo ilipokumbwa na Kimbunga katika maeneo ya mkoa wa Lindi.

Imetayarishwa na Mwandishi wetu, Idd Uwesu, Tanzania

XS
SM
MD
LG