Tangazo la hali ya dharura la Alhamisi limetokea siku hiyo hiyo ambapo mkuu wa ujumbe wa Umoja wa Mataifa katika jamuhuri ya Afrika ya Kati, Mankeur Ndiaye, alipotoa wito kwa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuongeza walinda amani nchini humo, akionya kwamba taifa hilo liko katika hatari kubwa ya kurudi nyuma katika suala la usalama na ujenzi wa amani.
Ndiaye amependekeza pia msaada wa kikanda na kimataifa utolewe kwa Jamuhuri ya Afrika ya Kati.
Rais wa zamani Francois Bozize alishutumiwa kuchochea ghasia baada ya mahakama ya katiba kupinga ugombea wake kwenye uchaguzi wa rais wa tarehe 27 Disemba, na wiki hii mahakama hiyo imemtangaza Touadera mshindi wa uchaguzi huo.