Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumanne, Aprili 23, 2024 Local time: 14:48

Elton John achangisha dola millioni sita kupambana na HIV Kenya


Sir Elton John
Sir Elton John

Mwanamuziki maarufu wa Uingereza Sir Elton John amechangisha dola millioni sita kwa ajili ya kupambana na virusi vya HIV na ukimwi nchini Kenya.

Mwanamuziki huyo alikusanya fedha hizo katika tamasha lililohudhuriwa na watu mashuhuri Jumatano kusini mwa Ufaransa.

Fedha hizo zilikusanywa kusaidia mpango wa kusambaza vifaa vya kujipima HIV kwa ajili ya vijana laki nne nchini Kenya.

Tamasha hilo lilihudhuriwa na watu kadha mashuhuri wakiwemo wanamuziki na wacheza sinema mashuhuri duniani.

Taasisi ya Elton John Foundation ilitangaza mwaka 2018 kuwa ina lengo la kupanua uwezo wa kugundua na kutibu uambukizaji wa virusi vya HIV, hasa Afrika, Kusini mwa jangwa la Sahara. Elton John alisema katika tamasha hilo ni muhimu kwa watu kuweza kujipima wenyewe kwa sababu wengi wanaona aibu kwenda katika vituo vya afya.

Mwimbaji huyo na mtunzi wa nyimbo, akiwa katika mapumziko wakati wa safari yake ya kuaga akipita sehemu mbalimbali duniani aliwakaribisha wanamuziki wa kizazi chake katika nyumba yake yakifahari iliyoko Cap d’ Antibes akiwemo Mwimbaji Chris Martin wa bendi ya Coldplay, mpiga gitaa wa bendi ya The Who, Pete Townshend, mcheza filamu Joan Collins na Taron Egerton, aliyecheza nafasi ya John katika filamu ya “Rocketman,”

Taasisi ya Elton John AIDS imechangia kiasi cha dola za Marekani milioni 450 katika miradi mbalimbali tangu ilipoanzishwa mwaka 1992, kwa mujibu wa maafisa wa taasisi hiyo. Sehemu kubwa ya fedha zinatokana na uchangishaji katika karamu za kila mwaka na minada mbalimbali huko Los Angeles na New York.

Imetayarishwa na mwandishi wetu, Washington, DC.

XS
SM
MD
LG