Ufafanuzi huu umekuja wakati kumekuwa na mhemko wa wachumi, baadhi ya Wakenya na viongozi wakikosoa hatua hiyo ya serikali ya kuamua kukopa shilingi bilioni 200 kutoka katika taasisi za fedha za kimataifa.
Kiongozi huyo bungeni ameungana na viongozi wengine akiwemo Makamu wa Rais William Ruto ambaye ametetea utashi wa serikali ya Kenya katika kuchukua mkopo huo pamoja na kuwepo wasiwasi kwamba deni la taifa linaongezeka kwa kiwango ambacho itashindwa kukilipa na mkopo huo unaweza kufikia mahali ikashindikana kuusimamia.
Mbunge huyo wa Jimbo la Garissa Mjini Aden Duale amesema kuwa nchi ya Kenya inauwezo wa kulipa deni hilo na kwamba kiwango cha deni ukikilinganisha na pato la ndani la taifa (GDP) ambalo hivi sasa limefikia asilimia 56, ni hasi na linaweza kulipika ukilinganisha na nchi nyingine. Pia Duale amesema kuwa Waziri wa Fedha Henry Rotich alilifahamisha bunge jinsi ambayo Kenya itarejesha mkopo huo.
Amesema kuwa kiwango cha deni la Marekani ukilinganisha na pato lake la taifa (GDP) ni kwa asilimia 100 wakati Japan deni lake liko katika asilimia 200 ya pato lake la taifa (GDP) na lile la Falme za Kiarabu (UAE) liko katika asilimia 185 ukilinganisha na pato lake la taifa, na hata hivyo uchumi wa nchi hizo unaendelea kukua.