Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Machi 29, 2024 Local time: 13:58

Chadema, CUF vyadai mchezo mchafu uchaguzi mdogo Dar es Salaam


Ramadhan Kailima
Ramadhan Kailima

Wakati wagombea ubunge wa Siha na Kinondoni Mkoa wa Dar es Salaam nchini Tanzania  wakiendelea kujinadi, vyama vya Chadema na CUF vimedai kuna mchezo mchafu unafanyika katika uchaguzi mdogo Kinondoni dhidi ya vyama vyao.

Vyama hivyo vimeeleza Jumapili kuwa baada ya mawakala wao kulazimishwa kula kiapo, mpaka sasa hawajakabidhiwa viapo vyao.

Jana Jumamosi kwa nyakati tofauti, mwenyekiti wa Chadema Wilaya ya Kinondoni, Waziri Muhuzi na mkurugenzi wa habari, uenezi na uhusiano wa umma wa CUF, Abdul Kambaya walisema endapo viapo havitatolewa katika muda muafaka mawakala wao wanaweza kushindwa kutekeleza majukumu yao ipasavyo. Hiyo wameongeza ni pamoja na kusimamia kura za ubunge na udiwani.

Vyanzo vya habari vimeripoti Jumapili kuwa Muhuzi alisema katika kata ya Hananasif, mawakala 50 wa Chadema kati ya 611 wa jimbo hilo walilazimisha kupewa viapo hivyo, huku Kambaya akibainisha kuwa mawakala wote wa CUF wamekubali kula kiapo bila kupewa viapo vyao, na hivyo watawasilisha malalamiko yao Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC).

Muhunzi amedai kuwa kitendo cha kuapa kimefanyika kinyume na kanuni za uchaguzi zinazoagiza wakala kuapa na kuondoka na kiapo chake.

Mvutano huo umeibuka ikiwa imepita siku mbili tangu NEC kuvitaka vyama vya siasa vinavyoshiriki uchaguzi huo mdogo unaofanyika Februari 17, kuwasilisha majina ya mawakala wao"

Mkurugenzi wa Uchaguzi wa NEC, Ramadhan Kailima amesema ili wakala akamilike, lazima awe na barua kutoka kwenye chama chake, ale kiapo na awe na barua ya utambulisho kutoka kwa msimamizi wa uchaguzi kwenda kwa msimamizi wa kituo.

Alipotafutwa jana kueleza kuhusu mawakala hao kunyimwa viapo, Kailima alisema vyama hivyo vina haki ya kuwasilisha madai hayo.

Hata hivyo, alifafanua kuwa kutokana na wingi wa mawakala, haikuwa rahisi kwa wasimamizi wa uchaguzi kusaini viapo vyao vyote kwa wakati mmoja.

XS
SM
MD
LG