Vyanzo vya habari vimesema kuwa Mhariri Mkuu wa Raia Mwema,Godfrey Dilunga, amesema taarifa ya kusitishiwa uchapishaji huo wameupata jana kupitia barua iliyotolewa na Maelezo. Serikali imelifungia kwa siku tisini gazeti hilo kwa madai ya kuandika habari za uongo dhidi ya Rais John Magufuli. Gazeti hilo hutolewa kila Jumatano. “Adhabu tuliyopewa ni kubwa kwetu, mara nyingi inapotokea tumeandika habari ambayo inaonekana ipo tofauti huwa wanatuita tunakaa tunaeleweshana na mambo mengine yanaendelea,” alisema. Amri hiyo ya kiutendaji imetolewa ikiwa ni siku 10 baada ya gazeti jingine la kila wiki la Mwanahalisi kufungiwa kwa kipindi cha miezi 24 (miaka miwili), kwa kile serikali inachodai kuwa ni mfululizo wa kukikiuka maadili, misingi ya sheria ya taaluma za uandishi wa habari, kuandika habari za uongo, uchochezi na kuhatarisha Usalama wa Taifa. Dilunga alipoulizwa kama walishawahi kupewa barua ya onyo alisema hawezi kuongelea suala hilo kwa kuwa angepaswa kutoa maelezo mengi kwa wakati huo. Alisema Ijumaa uongozi wa gazeti hilo umelazimika kukutana na kufanya kikao cha dharura ili kujadili suala hilo. Serikali imetoa tamko kuwa watanzania wakiufanyia mzaha upotoshaji wa taarifa na uchochezi katika zama hizi za Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (Tehama) amani na utulivu inayojivuniwa kwa miaka mingi vitapotea na kukaribisha maafa kama ilivyotokea kwingineko duniani. Baadhi ya nukuu katika toleo ni pamoja na kwamba "Wanaoishi kama malaika atawashusha waishi kama shetani”, suruali za zamani msizitupe mtazihitaji baadaye” na watakaobakia Dar es Salaam baada ya mwezi watakuwa wanaume kwelikweli” |
|