Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumanne, Aprili 23, 2024 Local time: 19:34

Mwanahalisi-Tanzania kumdai Naibu Waziri milioni 41


Saed Kubenea akitoka Mahakamani baada ya kesi mojawapo iliokuwa inamkabili kusomwa
Saed Kubenea akitoka Mahakamani baada ya kesi mojawapo iliokuwa inamkabili kusomwa

Wamiliki wa gazeti la mwanahalisi lililofungiwa na serikali wamemtaka Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni Sanaa na michezo Anastazia Wambura kulifungulia gazeti hilo au watakutana mahakamani.

Serikali imelifungia gazeti lao kwa kipindi cha miaka miwili kuanzia Septemba 19 mwaka 2017.

Waziri ametakiwa afungulie gazeti hilo ndani ya siku mbili kuanzia Jumatano vinginevyo watamfungulia mashtaka mahakamani.

Licha ya kwenda Mahakamani Mwanahalisi itamdai fidia ya Shilingi milioni 41 yeye Naibu waziri binafsi kwa kila chapisho ambalo halitachapishwa kutokana na kufungiwa gazeti hilo.

Kauli hiyo imetolewa Jumatano jijini Dar es salaam na mmoja wa wamiliki wa gazeti la Mwanahalisi Saed Kubenea katika mkutano wake na waandishi wa habari.

Tayari mwanasheria wao amepeleka barua rasmi Jumanne kwa naibu waziri kwa vile amelifungia gazeti hilo wakati kuna amri ya Mahakama Kuu ya Dar es Salaam ya kutolifungia gazeti hilo.

Hatua hii ni kuonyesha jinsi gani magazeti ya Mwanahalisi yanavyo sakamwa ikiwa pamoja na kufungiwa gazeti hilo wakati kuna amri ya Mahakama Kuu iliyokuwa tayari imetolewa na Jaji Bongole.

Pia kuna madai ya Mwanahalisi kuwa serikali imefungia gazeti bila ya kwenda mahakamani.

Katika kesi hiyo iliyofunguliwa na Mwanahalisi mshtakiwa wa kwanza alikuwa Mwanasheria Mkuu wa serikali, mshtakiwa wa pili ni Waziri wa Habari na mshtakiwa wa tatu msajili wa magazeti ambaye ni Mkurugenzi wa Maelezo.

Katika kesi hiyo vyanzo vya habari vimeeleza kuwa serikali imekata rufaa Mahakama ya Rufaa. Lakini Mkurugenzi wa Maelezo hakukata rufaa ikimaanisha kuwa alikuwa ameridhika na uamuzi wa Mahakama Kuu.

Serikali ya Tanzania ililifungia gazeti la Mwanahalisi kwa miaka miwili zuio ambalo pia linahusisha machapisho ya mtandaoni.

Gazeti hilo limefungiwa kwa kile kilicho arifiwa kuwa ni kuchapisha habari za uongo na uchochezi ambazo zinadaiwa kuwa zinaweza kuhatarisha usalama wa taifa hilo.

Sababu zilizopelekea kufungiwa gazeti hilo kunatokana na kuchapisha mlolongo wa habari ambazo zinasemekana kuwa za kichochezi ikiwemo yenye kichwa cha habari 'Tumwombee Magufuli au Tundu Lissu' iliyochapishwa katika toleo la 409 la tarehe 18-24 Septemba 2017 .

Miezi ya hivi karibuni vyombo vya habari vimekuwa vikifuatiliwa kwa ukaribu nchini Tanzania. Mwanzoni mwa 2017 Rais Magufuli alivionya vyombo vya habari 'visifikiri viko huru kwa kiwango hicho.'

XS
SM
MD
LG