Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Machi 29, 2024 Local time: 14:47

Afrika Kusini : Ramaphosa asema uporaji na vurugu ulikuwa umepangwa


Rais Cyril Ramaphosa
Rais Cyril Ramaphosa

Rais wa Afrika Kusini, Cyril Ramaphosa, Ijumaa amedai  uporaji na vurugu mbaya ambazo zimetikisa nchi hiyo kwa kipindi cha wiki moja sasa zilipangwa.

Amesema hayo alipowasili katika kitovu cha machafuko hayo ambayo yamepelekea maafa na uharibifu mkubwa wa mali tangu rais wa zamani wa nchi hiyo, Jacob Zuma, kujisalimisha kwa polisi na kuanza kifungo cha miezi kumi na mitano, gerezani.

Rais wa Afrika Kusini amesema : "Ni wazi kabisa kuwa matukio haya yote ya machafuko na uporaji yalichochewa. Kuna wachochezi. Kulikuwa na watu ambao walipanga. Waliyaratibu."

Waziri katika afisi ya Ramaphosa, Khumbu-Dzo Ntsh-Veni, aliwaambia waandishi wa habari kwamba, ingawa kwa kiasi kikubwa, hali ya utulivu, imerejea Johannesburg, hali katika jimbo la Kwazulu Natal "bado ni tete."

Unity Business South Africa (BUSA), kikundi kinachoheshimika, cha kutetea haki za wafanyabiashara kimeitaka serikali kutangaza katazo la kutotoka nje la saa 24 ili kudhibiti machafuko hayo kwa haraka.

Waandamanaji wakipora kutoka katika maduka huko Katlehong, South Africa, July 12, 2021. REUTERS/Siphiwe Sibeko
Waandamanaji wakipora kutoka katika maduka huko Katlehong, South Africa, July 12, 2021. REUTERS/Siphiwe Sibeko

Maduka na maghala ya kuhifadhia bidhaa yameporwa katika majimbo mawili na kusababisha hofu ya upungufu wa bidhaa jambo ambalo ni pigo kubwa kwa uchumi wa nchi hiyo. Watu wasiopungua 117 wamefariki, baadhi wakipigwa risasi na wengine kuuawa katika mkanyagano, wakati wa uporaji.

Kufuatia machafuko hayo takriban watu 2,200 wamekamatwa kama washukiwa wa makosa mbalimbali yakiwa ni pamoja na wizi.

Habari hii inatokana na vyanzo mbalimbali

XS
SM
MD
LG