Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Mei 04, 2024 Local time: 06:36

Kenya: Ruto afanya mabadiliko katika baraza la mawaziri, ateua makatibu na mabalozi wapya


Rais Ruto wa Kenya akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari katika Ikulu ya Nairobi, Mei 5, 2023. Picha na REUTERS/Moniah Mwangi
Rais Ruto wa Kenya akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari katika Ikulu ya Nairobi, Mei 5, 2023. Picha na REUTERS/Moniah Mwangi

Rais wa Kenya William Ruto Jumatano alifanya mabadiliko katika baraza lake la mawaziri, kuongeza wizara mpya, na kuwateua maafisa wapya kuchukua nyadhifa mbalimbali serikalini.

Mawaziri 8 ni kati ya waliohamishiwa kwa wizara nyingine huku majukumu ya Waziri Mkuu Musalia Mudavadi yakiongezwa, na idara moja kuondolewa kutoka kwa afisi yake.

Rais Ruto pia aliwateua makatibu wakuu kadhaa, mabalozi na manaibu wao, huku akiwahamisha wengine kuhudumu katika wizara au balozi mbalimbali.

Rais huyo alifanyia mabadiliko baadhi ya wizara, huku idara mbalimbali zikihamishwa.

Mudavadi aliteuliwa kama Waziri wa mambo ya Nje na masuala ya Diaspora, na wizara hiyo kuhamishwa na kuwa chini ya afisi yake, ambayo ilibuniwa baada ya uchaguzi wa mwaka jana.

Mabadiliko hayo yalifanyika kufuatia ukosoaji wa utendakazi wa baadhi ya maafisa waandamizi wa serikali ya muungano wa Kenya Kwanza.

Mwezi Mei, Ruto alikiri kwamba baadhi ya mawaziri walikuwa wamezembea na kuonya kuwa iwapo hawangejirekebisha, wangechukuliwa hatua.

Mabadiliko hayo yalikuwa muhimu, Ruto alisema, "kuboresha utendakazi na kuimarisha utoaji huduma kama ilivyoainishwa katika manifesto ya utawala".

Ruto amekabiliwa na msururu wa maandamano nchini kote kulalamikia gharama ya juu ya maisha na ongezeko la kodi tangu achukue mamlaka mnamo Agosti 2022.

Ni mara ya kwanza kwa Ruto kufanya mabadiliko kama hayo tangu aingie madarakani zaidi ya mwaka mmoja uliopita.

Mkuu wa utawala katika Ikulu Felix Koskei alitangaza Jumatano kwamba Mudavadi atachukua nafasi ya Alfred Mutua, ambaye amehamishiwa kwenye Wizara ya Utalii na Wanyamapori.

Waziri wa Biashara Uwekezaji na Viwanda sasa ni Rebecca Miano, akichukua nafasi iliyoshikiliwa na Moses Kuria ambaye sasa ndiye waziri mpya wa Utumishi wa Umma, Utendakazi na Uratibu wa Huduma

Aisha Jumwa amehamishiwa kwenye wizara ya Jinsia, Utamaduni, Sanaa na Turathi za kitaifa.

Mawaziri wengine waliohamishwa ni pamoja na Peninah Malonza, ambaye sasa ni Waziri wa masuala ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, Maeneo Kame na Ustawi wa kieneo.

Zacharia Njeru, aliyekuwa waziri wa Makazi, sasa ataongoza wiaza ya maji, usafi na unyunyiziaji, ambayo awali ilikuwa inashikiliwa na Alice Wahome.

Wahome sasa ndiye waziri mpya wa Ardhi, Makazi na Maendelo ya Mitaa.

Ruto aliingia madarakani kwa ahadi ya kutetea masilahi ya "wachuuzi" maskini, lakini wakosoaji wake walisema kupanda kwa gharama ya maisha, ushuru wa petroli na kiwango cha kodi inayaotozwa na serikali kitawaumiza.

Wakenya tayari wanatatizika kumudu bidhaa za kimsingi kama vile unga wa mahindi.

Forum

XS
SM
MD
LG