Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Mei 18, 2024 Local time: 10:15

Marekani yasema itaendelea kuunga mkono jeshi la raia


Waziri wa Ulinzi wa Marekani Lloyd Austin na Waziri wa Ulinzi wa Kenya Aden Duale wakipeana mikono baada ya kutia saini Mkataba wa Ushirikiano wa Ulinzi jijini Nairobi, Kenya Septemba 25, 2023. Picha na REUTERS/Monica Mwangi
Waziri wa Ulinzi wa Marekani Lloyd Austin na Waziri wa Ulinzi wa Kenya Aden Duale wakipeana mikono baada ya kutia saini Mkataba wa Ushirikiano wa Ulinzi jijini Nairobi, Kenya Septemba 25, 2023. Picha na REUTERS/Monica Mwangi

Marekani itaendelea kuyaunga mkono majeshi "yanayoongozwa na raia" barani Afrika, waziri wa ulinzi wa Marekani Lloyd Austin, alisema Jumatano akilaani mfululizo wa mapinduzi ya hivi karibuni wakati akielezea mkakati wa usalama wa Washington barani Afrika.

"Hiyo itabaki kuwa kanuni ya msingi ya kujihusisha kwa Marekani na washirika wetu wa Afrika," Austin alisema wakati wa hotuba yake katika mji mkuu, Luanda.

"Kwa hivyo tutaendelea kuwekeza kwa majeshi yenye weledi, yanayoongozwa na raia... Tutakuwa wazi kwa washirika wetu wakati taasisi zao za usalama hazifikii viwango hivyo vya kimataifa."

Austin hakuitaja nchi yoyote, lakini maoni yake yalionekana dhahiri anaizungumzia Niger, ambayo viongozi wa kijeshi walimpindua rais aliyechaguliwa kidemokrasia mwezi Julai na Marekani ina wanajeshi wapatao 1,100 nchini humo.

"Wakati majenerali wanapopindua matakwa ya watu na kuweka malengo yao juu ya utawala wa sheria, usalama unaathirika," alisema, akiwashutumu "watawala" ambao "wanahujumu chaguzi huru na za haki".

Mapema wiki hii, Austin alisema Marekani "itatathmini" hatua zake zitakazofuata katika mgogoro wa Niger baada ya Ufaransa kutangaza kuondoa wanajeshi wake kama walivyotakiwa na viongozi wa kijeshi.

Austin alikuwa Angola katika kituo chake cha mwisho cha ziara yake ya nchi tatu, ikiwa ni pamoja na kuzitembelea Djibouti na Kenya, kwa lengo la "kuimarisha ushirikiano" katika bara hilo, ambako China na Russia wameongeza ushawishi.

Niger ni miongoni mwa mataifa kadhaa yaliyopitia mapinduzi tangu 2020, pamoja na Burkina Faso, Guinea, Gabon na Mali.

Nchi hiyo tangu wakati huo imeielekea Moscow, ikiingiza mamluki kutoka kundi la Wagner.

"Afrika inastahili mambo mazuri kuliko watawala wa kiimla wanaouza bunduki kwa bei rahisi, kuingiza vikosi vya mamluki kama Kundi la Wagner, au kuwanyima nafaka watu wenye njaa duniani," Austin alisema, akiimanisha Kremlin.

Chanzo cha habari hii ni Shirika la habari la AFP

Forum

XS
SM
MD
LG