Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumanne, Machi 19, 2024 Local time: 08:55

Watu walikufa kwa sababu ya uzembe, wangeweza kuokolewa katika ajali ya ndege


Ndege ya Precision air iliyoanguka katika Ziwa Victoria Bukoba, Tanzania, November 6, 2022.
Ndege ya Precision air iliyoanguka katika Ziwa Victoria Bukoba, Tanzania, November 6, 2022.

Ripoti ya awali kuhusu uchunguzi unaoendelea kuhusu ajali ya ndege ya Precision nchini Tanzania inasema kwamba Maisha ya watu yangeokolewa endapo maafisa wa uokoaji wangeajibika kwa muda unaofaa.

Licha ya serikali kusema kwamba mawasiliano kati ya rubani na usimamizi wa uwanja wa ndege yalionyesha kwamba ndege ilikumbwa na usumbufu wa kutua kwa karibu dakika 20, hakuna hatua yoyote ilipangwa kuchukuliwa hata baada ya ndege kuanguka.

Watu 19 walifariki Novemba 6, wakati ndege ya precision yenye watu 43 ilipoanguka katika ziwa Victoria, Bukoba.

Wavuvi wanaotumia boti ndogo ndio waliokuwa wa kwanza kufika kwenye ndege hiyo na kusaidia kuokoa watu 24.

Ripoti inayodaiwa kuwa ya awali kuhusu uchunguzi huo, imekuwa ikisambaa kwenye mitandao ya kijamii. Kulingana na ripoti hiyo, kuna vifaa vya uokoaji kwenye uwanja wa ndege wa Bukoba, lakini wahusika hawakufika kusaidia katika uokoaji.

Polisi wa uokoaji walikosa oxygen, mafuta, walifika saa 5 baada ya ajali kutokea

Polisi wa kupiga doria baharini hawakupata taarifa kuhusu ajali hiyo, na walipopewa taarifa, walifika eneo la ajali saa tano baadaye bila ya Oxygen. Isitoshe boti la uokoaji halikuwa na mafuta ya kutosha kufanikisha shughuli hiyo.

Na baada ya ripoti kuenea kwenye mitandao ya kijamii, waziri wa habari, sayansi na Teknolojia Prof Makame Mbarawa ametetea serikali akisisitiza kwamba kwamba ilichukua kila hatua kuokoa Maisha, ikijiondolea lawama kwamba hali ya hewa ilibadilika ghafla na kwamba ndege ilizunguka kwa dakika 20 kabla ya kuanguka na kwamba zipo kanuni za kimataifa kuhusu uokoaji ambazo lazima zizingatiwe wakati wa ajali ya ndege.

“Nikweli kuwa mlango wa ndege iliyopta ajali ulifunguliwa na mhudumu wa ndege kwa msaada wa abiria. Hata hivyo, kama ripoti ya uchunguzi ilivyosema, wananchi waliokuwa wanafanya kazi shughuli za uvuvi, Jirani na eneo la ajali walifika eneo la ajali dakika 5 baada ya ndege kuanguka. Wananchi hao waliendelea na juhudi za kufungua mlango kwa nje. Hali hiyo ilisaidia kumpa ujasiri mhudumu wa ndege na abiria ndani ya ndege kufungua mlango huo baada ya kuona nje ya ndege kuwa kuna msaada ambao unaweza kuwasaidia.”

Serikali ya Tanzania imefutilia mbali ripoti inayosambazwa kwenye mitandao ya kijamii. Serikali inasisitiza kwamba hakuna mtu mwingine ana haki ya kutoa ripoti ya uchunguzi pasipo serikali.

Kiongozi wa chama cha Upinzani cha ACT Wazalendo Zitto Kabwe
Kiongozi wa chama cha Upinzani cha ACT Wazalendo Zitto Kabwe

“Serikali iombe msamaha kutokana na uzembe wa maafisa wake”

Mwenyekiti wa chama cha ACT Wazalendo Zitto Kabwe, ambaye ni miongozi wa watanzania waliosambaza ripoti hiyo kwenye mitandao ya kijamii, anasisitiza kwamba ripoti inayosambaa ni ya kweli na kwamba kilichotokea ni uzembe mkubwa kutoka kwa watu wenye jukumu la uokoaji, akisisitiza kwamba wanastahili kuajibishwa.

“Hiyo taarifa ni ya serikali na serikali imeituma kwenye vyombo vya kimataifa vinavyohusiana na usalama wa ang ana kama serikali haiwezi kuwaajibisha watu waliofanya uzembe katika uokoaji wa wananchi wetu, la chini zaidi inalostahili kufanya ni kusema wananchi samahani tulikosea, tulilala kazini. Angalau waombe msamaha. Watu wamekufa kwa uzembe, watu wangeweza kuokolewa,” amesema Kabwe.

Tangu ajali hiyo ilipotokea, Watanzania wamekuwa wakihoji namna shughuli ya uokoaji ilivyofanyika kiasi cha ndege kuvutwa na watu wa kawaida kwa Kamba.

XS
SM
MD
LG