Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Julai 27, 2024 Local time: 05:07

Watu wenye silaha wawateka wanafunzi 80 na waalimu watano Nigeria


Jimbo la Kebbi, Nigeria
Jimbo la Kebbi, Nigeria

Watu wenye silaha wamemuua afisa mmoja wa polisi na kuwateka nyara wanafunzi 80 na waalimu wa tano kwenye shule ya jimbo la Nigeria la Kebbi, ripoti ya Shirika la habari la Reuters imesema ikinukuu polisi na wakazi wa jimbo hilo.

Hilo ni shambulizi la tatu la utekaji nyara wa watu wengi katika kipindi cha wiki tatu kaskazini mwa Nigeria, viongozi wakisema vitendo hivyo vya utekaji nyara vinafanywa na majambazi wenye silaha wanaodai fidia.

Usman Aliyu, mwalimu kwenye shule iliyoshambuliwa anasema watu hao wenye silaha wamewachukua wanafunzi 80 wengi wao wakiwa wasichana.

Msemji wa polisi katika jimbo la Kebbi Nafiu Abubakar amesema watu wenye silaha walimuua afisa wa polisi na kumpiga risasi mwanafunzi ambaye anapatiwa matibabu kwa sasa.

Hadi siku ya Alhamisi polisi walikuwa hawajatangaza idadi kamili ya wanafunzi waliotekwa nyara.

Wazazi wa watoto wa shule ya Kiislam ya Salihu Tanko wakisubiri habari juu ya kutekwa kwa watoto wao huko Tegina, Nigeria, Juni 1, 2021.
Wazazi wa watoto wa shule ya Kiislam ya Salihu Tanko wakisubiri habari juu ya kutekwa kwa watoto wao huko Tegina, Nigeria, Juni 1, 2021.

Shambulizi hilo lilifanyika kwenye chuo kikuu cha serikali katika mji ulio mbali wa Birnin Yauri.

Msemaji wa polisi katika jimbo la Kebbi, Abubakar amesema maafisa wa usalama wanawatafuta wanafunzi na waalimu waliotekwa nyara katika msitu ulioko karibu.

Mashambulizi katika jimbo la kaskazini magharibi ni tofauti na vitendo vya uasi vinavyofanyika kaskazini mashariki, ambako kundi la Boko Haram liligonga vichwa vya vyombo vya habari mwaka wa 2014 lilipoteka nyara zaidi wa watoto wa shule wa kike 270 katika mji wa Chibok.

Chanzo cha Habari : Reuters

XS
SM
MD
LG