Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Julai 27, 2024 Local time: 04:56

Wabunge wa Jubilee Kenya wailaumu serikali


Chama cha mawakili nchini Kenya wakiandamana kushinikiza amri za mahakama ziheshimiwe
Chama cha mawakili nchini Kenya wakiandamana kushinikiza amri za mahakama ziheshimiwe

Wabunge wa chama cha Jubilee nchini Kenya wameilaumu serikali kwa kutoheshimu amri za mahakama.

Wabunge wa Jubilee Ijumaa waliingilia kati kupinga kitendo cha kukaidi amri za mahakama na hasa suala lenye utata la kuondolewa kwa nguvu nchini wakili machachari Miguna Miguna kutoka nchini na kurudishwa nchini Canada

Seneta Mithika Linturi na Mbunge wa Buuri Rindikiri Mugambi waliipongeza Mahakama Kuu baada ya Jaji Luka Kimaru kutoa uamuzi ukiitaka serikali kumrejeshea pasipoti ambayo haijamalizika muda wake Miguna na kwa kubatilisha amri ya Waziri wa Mambo ya Ndani Fred Matiang’i ya kumuondosha wakili huyo nchini.

Kwa mujibu wa vyanzo vya habari nchini Kenya wabunge hao wawili walipinga kitendo cha Jubilee wazi wazi kukaidi amri ya mahakama bila ya kujali kwamba wao wamedhaminiwa katika nafasi zao za ubunge na chama cha Jubilee.

Serikali ya Kenya hata hivyo imekata rufaa kupinga uamuzi wa Jaji Kimaru, wakisema kuwa kurudishwa kwa Miguna nchini ni kinyume kabisa na maslahi muhimu ya taifa.

“Ukiwa ni afisa, au waziri au afisa wa polisi na yoyote yule – unasema kuwa huwezi kufuata amri ya mahakama… kwa hili lazima tuseme hapana. Hatuwezi kuruhusu! Hatuwezi kukaa chini na kuruhusu Kenya ielekee kwenye udikteta.

Ikiwa kuna jambo lolote jingine tuko tayari kulipigania na tuko tayari kupambana nalo ni uhuru wa mahakama na kutoingiliwa kwa mahakama kwa sababu pale ambapo wananchi wa Kenya watapoteza imani na mahakama, itakaribisha mazingira ya udikteta na kuvunjika kwa amani nchini,” Seneta Linturi amesema.

Mbunge wa Buuri Mugambi alieleza masikitiko yake sawa na yale ya Linturi akisema kuwa hakuna mtu yoyote alioko juu ya sheria na Katiba ndio iliyo juu ya kila kitu.

“Uhuru ambao tumepewa na Katiba yetu hauwezi kutumiwa vibya na mtu yoyote kutoka upande wowote. Hakuna nafasi yoyote ya uongozi ambayo tunashikilia itaweza hivi sasa kuingilia mihimili mingine ya serikali,” Mugambi alisema.

XS
SM
MD
LG