Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumanne, Machi 19, 2024 Local time: 09:37

Unyonyeshaji : WHO yatangaza hatua 10


VENEZUELA-HEALTH/
VENEZUELA-HEALTH/

Shirika la Afya Duniani (WHO) linasema kunyonyesha watoto katika miaka miwili ya kwanza tangu kuzaliwa kutaokoa maisha ya zaidi ya watoto 820,000 walio na umri wa chini ya miaka mitano kila mwaka.

WHO imetoa muongozo mpya wa hatua 10 ambao unalenga kuhamasisha kunyonyesha watoto katika vituo vya afya kote duniani.

Shirika pamoja na idara ya Umoja wa Mataifa ya kuhudumia watoto (UNICEF) walizindua juhudi zilizojulikana kama Baby-Friendly Hospital mwaka 1991, program ya kujitolea ambayo inashawishi kina mama wapya kuwanyonyesha watoto wao.

Mashirika hayo mawili yanataka kupanua program hii kusudi unyonyeshaji watoto uwe ni kiwango cha kawaida cha huduma kwa watoto wote katika mahospitali yote, lengo likiwa ni kufanikisha hilo kwa asilimia 100.

Afisa ufundi katika WHO kwenye idara ya Afya ya Lishe na Maendeleo, Laurence Grummer-Strawn anasema muongozi huo wa hatua 10 unavishauri vituo vya afya jinsi huduma inavyotakiwa kutolewa kwa kina mama wapya na watoto wao.

“Inalenga kwenye masuala, kama vile kuwaweka mama na mtoto pamoja, ngozi kwa ngozi, haraka baada ya kujifungua, kuanza kumnyonyesha ndani ya dakika chache tu baada ya kuzaliwa. Ni kuhusu kuepuka matumizi ya maziwa ya unga mpaka kuwepo na sababu za kiafya kufanya hivyo.

Jambo jingine ambalo ni jipya katika hatua hizi 10 ni kwamba zinawahusu watoto wote. Kiini cha hatua hizi 10 pia zitatumika kwa watoto waliozaliwa mapema kabla ya muda kutimia, watoto uzito mdogo, watoto wagonjwa,” amesema Grummer-Starwn.

Grummer-Strawn anasema ulimwenguni ni asilimia 40 tu ya watoto walio na umri wa chini ya miezi sita ndiyo hupewa maziwa ya mama. Ameiambia VOA kwamba kwenye program hii huko barani Afrika kiwango chake ni kidogo mno kiko kwenye asilimia nne. Anasema hilo linatia wasi wasi kwa vile wanawake wachache wanapatiwa muongozo wanaohitaji kuhusiana na manufaa ya kuwanyonyesha watoto wao.

“Sisi tunaamini kwamba ukosefu wa kuwanyonyesha unachangia kwa kiwango kikubwa katika vifo vya atoto. Viwango vya vifo vya watoto wachanga havijashuka haraka sana kama vifo vya watoto wakati wa kujifungua. Na moja ya wasi wasi ni kwamba hatutoi huduma bora za lishe hasa kwa watoto wenye uzito mdogo na hivyo kuzungumzia hili katika kutoa huduma za mapema itakuwa ni njia bora ya kuzuia baadhi ya mambo hayo.

Watetezi wa haki wanasema kuwanyonyesha watoto kuna manufaa mengi mno. Wanasema inawalinda watoto wachanga kupata maambukizo na kupunguza vifo. Inaboresha ufahamu, utayari kwenda shule na mahudhurio. Wanasaema watoto na vijana wadogo ambao walinyonyeshwa maziwa ya mama walipokuwa watoto huenda wasiwe katika hatari ya kuwa na uzito mkubwa au unene wa kupita kiasi. Wanasema kuwanyonyesha watoto pia kunapunguza hatari ya saratani ya maziwa kwa kina mama.

XS
SM
MD
LG