Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Julai 27, 2024 Local time: 04:37

Polisi wataka Zitto athibitishe madai yake


Zitto Kabwe pamoja na wakili wake Albert Msando (kulia) wakiwasili Mahakama Kuu Dar Es Salaam
Zitto Kabwe pamoja na wakili wake Albert Msando (kulia) wakiwasili Mahakama Kuu Dar Es Salaam

Polisi Mkoa wa Kigoma wamemtaka Mbunge wa Kigoma Mjini, Zitto Kabwe (ACT-Wazalendo), kuthibitisha madai yake kuhusu mauaji ya wananchi zaidi ya 100 katika Wilaya ya Uvinza mkoani humo.

Zitto alikuwa amedai kuwa mauaji hayo yalitokea katika tukio la mapigano kati ya polisi na Wanyantuzu wilayani Uvinza, takribani siku 11 zilizopita.

Vyombo vya habari nchini Tanzania vimeripoti kuwa kiongozi huyo wa Chama cha ACT-Wazalendo, alidai kuwa katika tukio hilo, mbali na wananchi 100 kupoteza maisha pia askari wawili wanadaiwa kufariki dunia.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kigoma, Martin Ottieno, amekanusha madai hayo na kusema kuwa Zitto amepotosha kwa kiwango kikubwa habari hizo na kuwa anatafuta umaarufu, na hivyo apuuzwe.

Taarifa ya kamanda imeeleza ni wananchi wawili na askari wawili tu ndiyo waliopoteza maisha na si 100 kama alivyodai Zitto.

Kamanda Ottieno alimtaka mbunge huyo kufika ofisini kwake mkoani Kigoma na kuthibitisha taarifa anazozitoa kuhusiana na tukio hilo na kwamba awapeleke polisi katika eneo hilo ambalo amedai wananchi hao wameuawa na kupigwa na polisi.

“Tunamtaka Zitto aje Kigoma ili athibitishe taarifa anazozitoa na atupeleke kwenye hilo eneo ambalo wananchi wameuawa kwa kupigwa na polisi na atuonyeshe hayo makaburi,”alisema kamanda huyo.

XS
SM
MD
LG