Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Aprili 26, 2024 Local time: 05:44

COVID-19 : Nchi mbalimbali zachukuwa tahadhari kufunguwa shughuli za kibiashara


Polisi wamkamata mtu aliyekiuka amri ya kuondoka katika soko huko Bulawayo, Zimbabwe, March 31, 2020, ikiwa ni hatua ya kudhibiti maambukizi.
Polisi wamkamata mtu aliyekiuka amri ya kuondoka katika soko huko Bulawayo, Zimbabwe, March 31, 2020, ikiwa ni hatua ya kudhibiti maambukizi.

Nchi mbalimbali duniani zinachukuwa tahadhari katika kulegeza masharti ya watu kutotoka majumbani yaliyowekwa ili kuzuia kuenea kwa virusi vipya vya corona.

Zimbabwe

Rais wa Zimbabwe Emmerson Mnangagwa amesema shughuli za uchimbaji madini na viwanda vinaweza kufunguliwa tena, lakini ameongeza muda wa watu kutotoka nje kwa wiki mbili, ambao ulikuwa umalizike Jumapili.

Ujerumani

Serikali ya Ujerumani imeruhusu maduka madogo kufunguliwa Jumatatu, wakati ikiendeleza amri ya watu kutosogeleana.

Albania

Mamia ya biashara ndogo ndogo huko Albania zimeruhusiwa kuanza shughuli zao Jumatatu kwa mara ya kwanza katika mwezi huu. Boti za uvuvi na viwanda vya kusindika chakula vitaweza kuanza shughuli zake.

Sri Lanka

Sri Lanka imeondosha amri ya kutotoka nje kwa thuluthi mbili ya nchi hiyo, ikiwa na mpango wa kulegeza masharti ya kutotoka nje ifikapo Jumatano.

Norway

Wanafunzi nchini Norway walirejea mashuleni Jumatatu, wakati nchini Denmark wanafunzi wataanza kwenda shuleni Jumatano.

WHO

Mkuu wa Shirika la Afya Duniani Tedros Adhanom Ghebreyesus amesema “amefarijika” na namna nchi mbalimbali zinavyoendelea kupanga utaratibu wa kulegeza masharti ya watu kutokaribiana, lakini ametahadharisha kuwa “ni muhimu hatua hizi kutekelezwa kwa utaratibu.

New Zealand

Nchini New Zealand wametangaza Jumatatu mpango wao wa kumaliza amri ya kutotoka nje uliodumu kwa mwezi mzima ifikapo Aprili 27 ikifuata utaratibu. Waziri Mkuu Jacinda Ardern amesema baadhi ya amri zilizowekwa zitaendelea kulegezwa kwa kipindi cha wiki mbili wakati ambapo serikali yake itaendelea kutathmini hali ilivyo na kuamua iwapo waendelee shughuli zaidi kurejea katika hali ya kawaida.

Korea Kusini

Maafisa Korea Kusini pia wametaka tahadhari ichukuliwa baada ya kuondoa amri ya kutotoka nje wakati maambukizi machache mapya nchini humo yaliendelea kuonyesha kupungua.

“Tusiache kuendelea kuchukua tahadhari mpaka pale tutakapo hakikisha mgonjwa wa mwisho amepona,” Rais Moon Jae-in amesema.

Uingereza

Waziri mmoja wa serikali ya Uingereza amesema mabaa na migahawa vitaendelea kufungwa hata baada ya nchi hiyo kuanza kuelegeza masharti yakutotoka nje yaliwekwa nchi nzima ifikapo Mei 7, 2020.

Marekani

Biashara na shule katika sehemu nyingi za Marekani zimeendelea kufungwa, zikizusha maandamano dhidi ya magavana na amri walizotoa kwamba watu wakae majumbani na kujiepusha kukaribiana kwa kadiri wanavyoweza.

Vikundi hivyo vidogo vya waandamanaji ambavyo vingi vinamuunga mkono Trump vimejitokeza katika miji mikuu ya majimbo kadhaa, vikilalamika kuwa amri ya kutotoka majumbani inakiuka haki zao za kikatiba.

Rais Trump

Rais Trump amesema Jumapili katika mkutano wake wa kila siku anaoeleza taifa juu ya hali ya virusi vya corona baadhi ya magavana “wamekwenda mbali zaidi” na amri zao na watu wanahaki ya kuandamana kupiga hilo. Lakini amesema yote hayo kiukwelihayajalishi mwisho wa siku kwa sababu majimbo hayo yataanza kurudi katika hali ya kawaida.

Baadhi ya magavana wanasema kuwa majimbo yao bado kabisa hayako tayari kurejea katika hali ya shughuli za kawaida.

Gavana wa Maryland

“Tunapeleka ujumbe wenye kukinzana kwa magavana na wananchi, kama kwamba tupuuze sera na mapendekezo (yanayotolewa na wataalam wa afya) wa serikali kuu,” Gavana wa Maryland Mrepublikan Larry Hogan amekiambia kipindi cha “Hali ya Taifa” : kituo cha televisheni cha CNN Jumapili.

Mdemokrat Jay Inslee wa Washington amesema ujumbe wa Trump kwamba majimbo yaanze shughuli za kawaida ni “hatari.”

White House

Kadhalika, Mjumbe wa kikundi kazi cha White House kinacho shughulikia maambukizi ya virusi vya coronaSeema Verma amesema vituo vya kulea watu wazima Marekani vinalazimika hivi sasa kutuma ripoti kunapokuwa na maambukizi ya COVID-19 ya wazee hao katika vituo hivyo na maambukizi ya wanafamilia kwa kuripoti maambukizi hayo moja kwa moja kwa Idara za afya za serikali kuu.

Watu wazima ndiyo hasa wanakabiliwa na hatari ya maambukizi ya virusi vya corona na vituo vya kulea watu wazima siyo tu Marekani, lakini pia katika nchi nyingine, vimekosolewa kwa kutokuwa wa wazi kuripoti maambukizi ya COVID-19.

XS
SM
MD
LG