Nchini Kenya na hasa katika mji mkuu wa Nairobi, mvutano unaendelea kati ya madereva wa texi wa kitambo na wale wanaofanya biashara hiyo kutumia teknologia ya kisasa ya kimitandao kujipatia wateja maarufu kupitia UBER.
Mwezi uliopita, texi moja ya UBER ilichomwa moto na watu walioshukiwa kuwa wamiliki wa texi za kawaida. Texi nyingine ya kampuni hiyo imechomwa moto siku ya Jumanne mwezi mmoja tu baada ya tukio la awali.
Haya yamejiri licha ya juhudi za Serikali za kuleta uwiano baina ya wafanyabiashara wa magari ya texi. Tukio hilo la hivi karibuni limechochea hisia na maoni mbali mbali hasa kutoka kwa wateja wanaotumia huduma za texi.
Kwenye gazeti la Standard, Mill Polo anasema kuwa madereva wa texi wa mfumo wa kale wanatoza nauli kubwa inayofanya maisha kuwa magumu kwa kila mmoja. Book Runner anasema "tishio la madereva wa texi la kufanya mgomo dhidi ya kampuni ya UBER ni upuzi tu. Hao wanaonekana kuishi kwenye karne ya 20. Ni vyema wafahamu mambo yamebadilika."
Shark Attack anasema kuwa ghasia zinazotekelezwa na wanatexi hao wa kitambo ni kama mateke ya mwisho ya farasi anaekaribia kufa. Tukiwa tungalia nchini Kenya ni kwamba chama cha upinzani cha mrengo wa CORD kimelaumu chama tawala cha Jubilee na kusema kuwa kimeshirikiana na tume ya huru ya uchaguzi na mipaka IEBC kuhujumu juhudi zake za mradi wa OKOA KENYA ulionuia kurekebisha katiba kwa madai ya kuimarisha uongozi nchini.
Wana CORD kulingana IEBC, wameshindwa kujipatia saini milioni moja kutoka kwa wapiga kura zilizohitajika kuleta marekebisho hayo. Wengi wametoa maoni yao kuhusu swala hilo. Kwenye mtandao wa Twitter, Mrs. M anasema wakenya ndio wenye uwezo wa kuokoa nchi yao, tumechoka na sarakasi za viongozi waliochoka. Rein anashauri chama cha CORD kutumia nguvu walizo nazo kujiandaa kwa uchaguzi wa mwaka ujao (2017) kinyume na kudai kuokoa Kenya. Pkihoi anasema wengine wanaodai kuokoa Kenya wamekuwa uongozini kwa karibu miaka 20. Walipoteza nafasi ya kuokoa Kenya basi.