Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Aprili 25, 2024 Local time: 12:44

Tanzania, Uganda zasaini mkataba wa bomba la mafuta


Rais Museveni na Rais Magufuli
Rais Museveni na Rais Magufuli

Mkataba wa Ujenzi wa Mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi la kutoka Hoima nchini Uganda hadi Tanga nchini Tanzania umekamilika.

Kwa mujibu wa vyanzo vya habari nchini Uganda ujenzi huo utahusisha bomba lenye urefu wa Kilometa 1,443, uliokadiriwa kugharimu zaidi ya Dola za Marekani Bilioni 3.55.

Mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi kutoka Hoima, Uganda hadi Tanga, Tanzania, unatarajia kuinua uchumi wa nchi hizi mbili. Katika mchakato wa ujenzi wake, zaidi ya watu 10,000 wanatarajiwa kunufaika na ajira

Mkataba huo ulisainiwa mjini Kampala, Uganda jana baina ya Waziri wa Katiba na Sheria wa Tanzania, Profesa Palamagamba Kabudi na Waziri wa Nishati wa Uganda, Irene Muloni.

Tukio hilo limefanyika siku chache baada ya Rais John Magufuli wa Tanzania na Rais Yoweri Museveni wa Uganda, kutia saini tamko la pamoja la kukamilika kwa majadiliano ya mkataba huo, Ikulu Dar es salaam.

Rais Magufuli siku za karibuni aliuelezea mradi huo kuwa ni mkubwa, kwa kuwa Uganda imegundua shehena kubwa ya mafuta katika eneo la Hoima kiasi cha mapipa bilioni 6.5.

Waziri wa Sheria na Katiba wa Tanzania, Profesa Kabudi wakati akisaini mkataba huo alisema Tanzania inathamini uwepo wa mradi huo na imejipanga kuhakikisha unatekelezwa kwa mafanikio.

Naye Waziri wa Nishati na Madini wa Uganda, Irene alisema Uganda imeamua kusafirisha mafuta yake kupitia bandari ya Tanga kutokana na Tanzania kukidhi matakwa yenye faida za kiuchumi na kuzinufaisha nchi zote mbili.

XS
SM
MD
LG