Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumanne, Aprili 23, 2024 Local time: 13:41

Mafuriko yaua watu wasiopungua 14 eneo lililopigwa na tetemeko Uturuki


Watu wakiokolewa kutoka katika mafuriko kutokana na mvua kubwa huko Sanliurfa, Uturuki, March 15, 2023
Watu wakiokolewa kutoka katika mafuriko kutokana na mvua kubwa huko Sanliurfa, Uturuki, March 15, 2023

Mafuriko yameua watu wasiopungua 14 Jumatano wanaoishi katika mahema na nyumba za makontena katika eneo lililopigwa na tetemeko la ardhi Uturuki, na kuongeza shinikizo kwa Rais Recep Tayyib Erdogan kuelekea uchaguzi muhimu.

Watu kadhaa walichukuliwa na maji yaliyokuwa na kasi kubwa, ambayo yaliigeuza mitaa kuwa ni mito yenye matope katika maeneo yaliyopigwa na tetemeko la ardhi lenye ukubwa wa 7.8 kwa kipimo cha rikta.

Zaidi ya watu 48,000 walifariki nchini Uturuki na takribna 6,000 nchini Syria katika janga la Februari 6, lililokuwa na maafa makubwa zaidi katika zama hizi.

Maelfu ya walionusurika katika tetemeko la Uturuki wamehamishwa katika mahema na nyumba za makontena kote katika eneo la maafa, ambalo linahusisha majimbo 11 kote kusini mashariki mwa Uturuki.

Mvua kubwa zilipiga katika eneo hilo Jumanne na idara ya hali ya hewa inatarajia mvua hizo zitaendelea hadi Jumatano jioni.

Maafisa wa Uturuki walisema mafuriko hayo yameua watu 12 huko Sanliurfa, kiasi cha kilomita 50 kaskazini mwa mpaka wa Syria.

Watu wawili, akiwemo mtoto wa mwaka 1, pia walifariki katika mji wa karibu wa Adiyaman, ambapo watu watano hawajapatikana.

Picha zilionyesha maji yakizoa magari na kufurika katika nyumba za muda zilizoandaliwa kwa ajili ya waathirika wa tetemeko la ardhi.

Chanzo cha Habari hii ni shirika la habari la AFP

XS
SM
MD
LG