Na Saleh Mwanamilongo
MwanamuzikiKoffi Olomide amefikishwa mahakamani mjini Kinshasa baada ya kukamatwa na polisi mapema Jumanne, na kufunguliwa mashitaka baada ya kufukuzwa nchini Kenya kufuatia kumpiga teke mchezaji densi wake wa kike.
Mwendesha mashitaka wa mahakama ya Kinshasa ameomba Olomide ahukumiwe kifungo cha miezi 18 jela, lakini hakimu ameahirisha kikao Jumanne na kuamuru Koffi ashikiliwe rumande mjini Kinshasa.
Olomide alikamatwa nyumbani kwake mapema Jumanne na maafisa wa polisi zaidi ya sitini waliokwenda nyumbani kwake katika eneo la kifahari la Mont Fleury kusini mwa jiji la Kinshasa. Olomide alikataa kutii amri ya polisi,na kwa hiyo kukamatwa kwa nguvu na kufungwa pingu. Olomide aliwambia waandishi habari kwamba amedhalilishwa kwa kufanyiwa hivyo kama mwizi ama mwendawazimu.
Baada ya kufikishwa mbele ya jaji, mwendesha mashataka amemuelezea Olomide kuwa ni mhalifu sugu. Kwa hiyo mwendesha mashataka wa mahakama ya Kinshasa aliomba mwanamuziki huyo wa rumba apewe kifungo cha miezi kumi na minane jela.
Olomide alihojiwa mahakamani kwa kwa masaa kadha huku wandishi habari na wafuasi wake wakipigiwa marufuku kuhudhuria. Kwenye video inayomuonyesha akiwa kwenye ofisi ya mwendesha mashitaka Koffi Ololide aliomba apewe heshima yake kama mtuhumiwa ambaye bado hana hatia yeyote.
Kukamatwa kwa mwanamuziki huyo wa rumba kumefuatia malalamiko ya mbunge wa Kinshasa Zacharie Bababaswe na vilevile Jeanine Mabunda mshauri wa maswala ya wanawakekwenye ofisi ya rais Joseph Kabila. Koffi Olomide alirejea mjini Kinshasa Jumamosi asubuhi baada ya kufukuzwa na serikali ya Kenya baada ya video iliomuonyesha akimpiga teke mmoja wa wachezaji densi wake.
Mara alipowasili kwenye uwanja wa ndege wa Kinshasa, Olomide alizomewa na raia waliokuwepo. Kwenye mahojiano yake na televisheni ya kitaifa Juma pili, Olomide aliomba msamaha wa dhahiri kwa rais Joseph Kabila, mkewe na watoto wake na vilevile Wakongomani wote kutokana na kisa hicho. Koffi alisema kwamba ameona sifa yake imeharibika vibaya.
Koffi amekuwa na sifa mbaya ya kuwapiga watu wakiwemo wake zake, wacheza densi wake na aliwahi hata kumpiga meneja wake mwaka wa 2012.
Kufukuzwa kwake nchini Kenya kulikaribishwa vyema na wakongomani ambao walivamia mitandao ilikuomba serikali ya Kongo imfungulie kesi. Olomide aliyekuwa miaka ya nyuma rafiki wa karibu wa Papa Wemba lakini uhusiano wao uliharibika na kusababisha Olomide kutohudhuria mazishi ya Wemba mwezi Mei.
Wanamuziki wenzake wanamuelezea kuwa mtu mchokozi, na asiyejuwa kuishi na watu vizuri. Mara nyingi mwenyewe amejiita "Makila Mabe" inayomanisha kwa kiswahili mtu mwenye damu mbaya.