Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Aprili 25, 2024 Local time: 04:51

Kiongozi wa Hong Kong aahidi kuchukuwa hatua kali zaidi kuzima vurugu


Waandamanaji wakusanyika katikati ya Jiji la Hong Kong, China Novemba 11, 2019.
Waandamanaji wakusanyika katikati ya Jiji la Hong Kong, China Novemba 11, 2019.

Kiongozi wa Hong Kong ameahidi Jumatatu “kufanya kila analoweza” kumaliza maandamano yanayofanyika dhdi ya serikali yaliyovuruga jiji hilo kwa zaidi ya miezi mitano, kufuatia siku moja ya vurugu ambayo mtu mmoja aliuawa na mwengine kuchomwa moto.

Kwa mujibu wa Shirika la Habari la AP kunauwezekano kuwa Matamko ya Carrie Lam yakachochea dhana ya kuwa hatua kali za kisheria na operesheni za jeshi la polisi zitatumika kuzuia waandamanaji.

“Sitaki kutoa maelezo zaidi, lakini nataka kuweka bayana kuwa tutafanya kila tuwezalo kutafuta njia itakayo maliza vurugu Hong Kong kwa haraka iwezekanavyo,” Lam amewaambia waandishi wa habari.

Pia Lam amekataa kuridhia matakwa ya waandamanaji kufikia suluhisho la kisiasa.

“Kama kuna matarajio yoyote kwamba kwa kuendeleza uvunjifu wa amani, Serikali ya Hong Kong itasalimu amri kwa shinikizo kufikia kile kinachoitwa madai ya kisiasa, ninasema wazi na kwa sauti kubwa hapa: Hilo halitatokea,” Lam amesema, akitumia herufi za mkato za Mkoa Maalum wa Utawala (SAR), inayomaanisha kuwa hadhi ya jiji hilo ni eneo la ardhi ya China lenye mamlaka yake.

Kuna uwezekano kuwa vurugu za Jumatatu zikapelekea kuamsha hisia mpaya Hong Kong baada ya mwanafunzi aliyeanguka wakati wa maandamano ya awali kufariki kutokana na majeraha Ijumaa na jeshi la polisi liliwakamata wabunge sita wanaounga mkono demokrasia mwisho mwa wiki kwa tuhuma za kuzuia shughuli za bunge wakati wa mkutano uliokuwa na vurugu Mei 11. Wote waliachiwa kwa dhamana.

Chama tawala cha Kikomunisti cha China kimeeleza kitajaribu kutafuta njia ya kupitisha sheria dhidi ya wachochezi katika ardhi yake, baada ya hatua hiyo kusitishwa siku za nyuma kwa sababu ilipingwa na umma.

Wakati Beijing imekanusha ripoti zinazoeleza kuwa huenda ikamuondoa Lam mwakani, chama hicho wiki iliyopita kimetoa tamko kikisema “itaboresha” mfumo wa kuwaweka na kuwaondoa viongozi wa ngazi ya juu wa Hong Kong.

Katika picha za video zilizosambazwa, afisa wa polisi anaonekana akiwarushia risasi waandamanaji katika makutano ya barabara Jumatatu asubuhi, kisha akimlenga bunduki muandamanaji aliyekuwa amejifunika akimfuata.

Wakati wawili hao wakihangaika, mwandamanaji mwengine akiwa amevaa nguo nyeusi anamkabili, ambaye afisa huyo anamlenga na bunduki. Anapiga bunduki na risasi inampata tumboni mwandamanaji wa pili ambaye anaanguka ardhini. Afisa huyo inaelekea anapiga tena bunduki wakati mwandamanaji watatu anayejiunga na mapambano.

Muandamanaji aliyekuwa amevaa vazi jeupe anafanikiwa kukimbia, na kuruka katika ngazi zilizokuwa karibu, na afisa wa polisi na mwenzake wanawashikilia wale waandamanaji wawili waliokuwa wamewaangusha chini.

Polisi wanasema kuwa muandamanaji mmoja ndio aliyekuwa amepigwa na risasi na anafanyiwa upasuaji hospitali. Msemaji wa uongozi wa Hospitali ya Hong Kong amesema mtu huyo hali yake mbaya lakini hakutoa maelezo zaidi.

Hii ni mara ya pili muandamanaji anapigwa risasi tangu maandamano hayo yaanze mapema mwezi Juni, japokuwa polisi mara kwa mara wamekuwa wakitoa silaha za moto kuzuia mashambulizi ya waandamanaji. Zaidi ya watu 3,300 wamekamatwa katika maandamano hayo.

Maelezo machache yanapatikana kuhusu tukio la uchomaji moto katika eneo la jirani la Ma On Shan. Picha za video zilizopostiwa katika mitandao zinaonyesha aliyechomwa moto akibishana na kundi la vijana kabla ya mmoja wao kumwagia mafuta na kuwasha moto.

Imetayarishwa na mwandishi wetu, Washington, DC

XS
SM
MD
LG