Kitu ambacho kimewapa moyo watu wa kabila hili ni baada ya safari ndefu ya kutafuta haki zao za kupiga kura, mwaka huu kwa mara ya kwanza watashiriki uchaguzi mkuu Agosti.
Uhuru Kenyatta
Akiwakabidhi zaidi ya wamakonde elfu 4 vyeti vya uraia, vitambulisho vya kitaifa na vyeti vya kuzaliwa, rais Uhuru Kenyatta amesema jamii hiyo kwa sasa itashirikishwa katika maendeleo na ajira zinazotolewa na serikali ikiwemo vikosi vya usalama.
Wananchi hawa baada ya kupokea vyeti vya uraia na vitambulisho vya kitaifa na kadi za kupiga kura hawatakuwa tena na pingamizi ya kushiriki katika mchakato wa kidemokrasia wa kutafuta viongozi wao.
Maelfu waridhika
Kwa mujibu wa mwandishi wetu hatua hii imewafurahisha zaidi ya wamakonde elfu 4 wanaoishi nchini Kenya, baada ya serikali kuwapa vitambulisho na vyeti vya uraia.
Mama Amina Kassim Magoma pamoja na wenzake hawakuficha furaha yao huku wakiahidi kuiunga mkono serikali katika uchaguzi mkuu mwaka huu.
Hii ni baada ya shughuli ya usajili wa jamii hiyo inayojumuisha kabila la 43 nchini Kenya, iliyofanyika mwezi Oktoba mwaka jana kufuatia maandamano ya jamii hiyo kutaka uraia katika ikulu ya rais jijini Nairobi.
Amwagiza waziri
Mwandishi wa VOA mjini Mombasa anasema rais Uhuru Kenyatta amemwagiza Waziri wa Usalama wa Ndani kushughulikia suala la uraia wa makabila yalikuwa bado hayatambuliwi.
Hata hivyo jamii za warundi, wapemba na wanyarwanda walioshiriki maandamano ya kutafuta uraia pamoja na wamakonde siku za nyuma wamelalamika kuwa zoezi hili la usajili limewatenga.
Mzee Julius Kiza na mama Stella Kilinga hawakuficha ghadhabu zao wakisikitika kwamba wao hawakuingizwa katika mchakato huo.
Lakini viongozi wa kisiasa kusini mwa pwani ya Kenya wanakoishi wapemba wengi wakiwa katika shughuli za uvuvi wameiomba serikali kusikiliza kilio cha jamii hiyo.
Imetayarishwa na mwandishi wetu Amina Chombo, Kenya.