Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Aprili 19, 2024 Local time: 07:47

Imani za uchawi, Ukame zachochea ghasia Malawi


Wananchi wa Malawi wasimama katika mstari kusubiri chakula cha msaada kinachotolewa na Umoja wa Mataifa Februari 3, 2016.
Wananchi wa Malawi wasimama katika mstari kusubiri chakula cha msaada kinachotolewa na Umoja wa Mataifa Februari 3, 2016.

Hali ya ukame nchini Malawi inaelezewa hivi sasa inachochea kuibuka kwa ghasia na shutuma za uchawi.

Maeneo ya kusini mwa Malawi ndiyo ambayo yamekumbwa zaidi ya kipindi kikavu na hivyo kuibua ghasia za makundi dhidi ya wakazi wa baadhi ya vijiji ncini humo.

Mamlaka ya Malawi haraka imejibu kwa kulaani mashambulizi hayo na kuzima shutuma hizo wakisema ni habari za uongo.

Januari 29 mwaka huu, ilikuwa ni siku mbaya sana kwa Aidah Waisonina kamwe hataisahau. Yeye ni mkazi wa kijiji cha Nthambula nchini Malawi katika wilaya ya kusini ya Phalombe.

Anasema ilikuwa ni nyakati za jioni na walikuwa ndiyo kwanza wanataka kuanza kula chakula mara ghafla wakaona kundi la vijana wa kiume wenye silaha waliokuwa wanaelekea nyumbani kwake.

“Nilihofia maisha yangu na haraka nilikimbilia msituni. Nikiwa huko niliona kundi la watu wakichoma moto nyumba kadhaa.”

Waisoni ni miongoni mwa wana vijiji wanane ambao walilengwa siku hiyo wakishutumiwa kuwa walikuwa wakizuia mvua kunyesha kwa kutumia uchawi.

Polisi wanasema kumekuwepo na uvumi kama huo ambao ulisambaa katika sehemu nyingine wilayani humo, lakini hakuna ghasia nyingine ambazo zimeripotiwa.

Wana vijiji wanasema eneo hilo halijapata mvua tangu mwezi Desemba.Mazao yamenyauka, na hivyo kuongeza khofu ya njaa.

Kundi la watu walivamia na kufanya wizi katika nyumba ya mganga wa jadiJameson Maideni mwenye umri wa miaka 76.

Maideni anasema alishangazwa na shutuma hizo kwa sababu mahindi shambani kwake yamenyauka kwa sababu ya ukame. Anasema angewezaje kuizuia mvua na yeye mwenyewe hana kitu chochote cha kula?

Takwimu za karibuni kutoka wizara ya Kilimo zinaonyesha kwamba zaidi ya wakulima 700,000 wanatarajiwa kupoteza takriban asilimia 40 ya mavuno yao mwaka huu kwa sababu ya mvua chache. Wakulima wameshauriwa kupanda mapema endapo mvua zitanyesha basi kuna mazao shambani.

Polisi wanasema wamewakamata watu sita kuhusiana na shambulizi hilo na inaendelea kuwasaka wengine ambao wamekimbilia nchi jirani ya Msumbiji.

Msemaji wa kituo cha polisi huko phalombe, Innocent Moses ameiambia VOA kuwa uchunguzi wao wa awali umebaini kwamba ghasia zinahusiana na mivutano ya kichifu ambayo haijapatiwa ufumbuzi. Anasema wana jamii wanachukulia fursa ya ukame na kuingiza dhana za uchawi.

Phalombe ni wilaya ile ile ambako watu saba waliuawa na kundi la watu waliokuwa wamekasirika mwaka jana kutokana na uvumi wa imani za kishirikina na mashetani kushambulia wakazi.

Mkuu wa kijiji cha Nthambula ambaye naye anaitwa Nthambula alizungumza na VOA na kusema hakuna mtu hata mmoja ambaye anazuia mvua isinyeshe. “Hizo ni mbinu zinazo tumiwa na watu wachahe ili kufanya wizi wa mali za watu,” ameongezea.

XS
SM
MD
LG