“Kutokana na Tume kuhakikishiwa na vyombo husika vya serikali na vyombo vya usalama kuhusu uchaguzi, zoezi hilo litafanyika kama ilivyopangwa Alhamisi, Octoba 26,” amesema mkuu wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka, Wafula Chebukati.
Lakini kiongozi wa upinzani Kenya, Raila Odinga, ambaye alijitoa katika kinyang’anyiro hicho cha marejeo ya uchaguzi mapema Octoba, ametangaza “harakati za vuguvugu” ya kupinga uchaguzi Jumatano.
Odinga amewasisitizia wafuasi wake kuwa “waangalifu wanapokutana na kaka na dada zao.”
“Mnatakiwa msiwashambulie, waelimisheni juu ya dhuluma zinazotukabili sote,” amesema, akieleza kuwa chama cha NASA kitaendelea kuhamasisha nguvu zinazotaka maendeleo ili kwamba uchaguzi huru, haki na unaostahiki uandaliwe katika kipindi cha siku 90.
Mapema Jumatano, Jaji Mkuu David Maraga amesema kuwa majaji wawili tu wa Mahakama ya Juu walikuwepo katika kupiga kura kuahirishwa kwa uchaguzi siku moja kabla, ambapo idadi hiyo ilikuwa haijafikia majaji watano wanaotakiwa kufanya uamuzi huo.
Tume ya Uchaguzi Kenya imesema kuwa uteuzi wa maafisa wake uliofanyika hivi karibuni ni halali na wataendelea kuendesha uchaguzi mpya wa urais Alhamisi.
Uchaguzi wa Alhamisi ni wapili kufanyika mwaka huu nchini Kenya kumchagua rais. Mahakama ya Juu ilibatilisha matokeo ya uchaguzi Agosti 8 kwa sababu ilisema kulikuwa na dosari na ukiukaji wa sheria katika kupeperusha matokeo.