Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Machi 29, 2024 Local time: 15:47

DRC: Wapiganaji waingia mjini Bunia na kuondoka


Ramani ya Bunia, DRC
Ramani ya Bunia, DRC

Takriban wapiganaji 100 waliojihami kwa sialaha nzito nzito, wameingia katika mji wa Bunia mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo na kuondoka.

Hatua hiyo ya kuingia kwao mjini kunaripotiwa kuwa hatua ya kuonyesha nguvu zao na kwamba hawaridhishwi na namna mchakato wa kutafuta amani unavyoendeshwa.

Wapiganaji hao kutoka kundi la CODECO, walikuwa wamevalia utepe kwenye vichwa vyao ili kujitambulisha kwa urahisi.

Walizingira gereza la Bunia na kutaka wenzao waliokamtwa kuachiliwa huru.

Haijabainika sababu zilizopelekea maafisa wa usalama kutozuia kundi hilo la wapiganaji linaloshutumiwa na Umoja wa Mataifa kwa mauaji, kuingia mjini humo. Hakuna mashambulizi yameripotiwa.

Baada ya masaa kadha ambapo walifanya pia mazungumzo na maafisa wa jeshi wapiganaji hao waliondoka mjini humo na kurudi porini.

CODECO ni mojawapo ya makundi wa wapiganaji yanayofanya mashambulizi yake mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, yakidai kupigania ardhi na kulinda mali ya eneo hilo.

Video kwenye mitandao ya kijamii inaonyesha wanajeshi wa serikali ya DRC wakiwazuia watu kutowasongea wapiganaji hao waliojihami kwa bunduki na silaha za kurusha roketi na mapanga

Kundi hilo la CODECO, kutoka jamii ya Lendu, linashutumiwa na umoja wa mataifa kwa mauaji, kukata watu vichwa, unajisi na matendo mengine mabaya dhidi ya binadamu.

Msemaji wa jeshi la DRC Jules Ngongo, amesema kwamba hali ilikuwa imedhibitiwa na kwamba “walikuwa hawana hatari yoyote kando na kutaka kupewa ulinzi na jeshi na kutaka wenzao kuachiliwa huru kwa wenzao walio gerezani.”

Mnamo mwezi July, serikali ya DRC ilituma wajumbe kadhaa ikiwemo waliokuwa wapiganaji kuwashawishi wapiganaji hao wa CODECO kujisalimisha na kuacha vita.

Baadhi ya viongozi wa CODECO walikubali kuacha vita mwezi Agosti, japo haijabainika iwapo hatua hiyo itamaliza vita kwa sababu kundi hilo liligawanyika katika makundi kadhaa baada ya kuuawa kwa kiongozi wao.

Imetayarishwa na mwandishi wetu Kennes Bwire, Washington, DC

XS
SM
MD
LG