Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Machi 29, 2024 Local time: 08:54

Wabunge wa Somalia wakimbilia Kenya


Mapigano yanayongozwa na wanaharakati wakislamu wenye itikadi kali yamewapelekea wabunge 15 wa Somalia kukimbilia nchi jirani ya Kenya, wakihofia maisha yao.

Wabunge hao waliwasili Nairobi mapema wiki hii wakisema hali ni ya hatari na hawaamini serikali ya mpito inaweza kuendelea kupambana na vikosi vya wanamgambo wa al-Shabab na washirika wao bila ya msaada wa kigeni.

Kuna zaidi ya wabunge 280 walobaki huko Mogadishu ili kuhakikisha miswada inapitishwa, kwani inahitajika wabunge 250 kati ya wabunge 550 wa bunge la mpito kuweza kuwa na majadiliano yeyote.

Wakati huo huo mwandishi wa Sauti ya Amerika Mwai Gikonyo, anaripoti kwamba zaidi ya watu 100 waliojeruhiwa vibaya kutokana na majeraha ya risasi, waliwasili Nairobi na kupelekwa katika hospitali mbali mbali za mji huo wakiwa chini ya ulinzi mkali.

Balozi wa Somalia mjini Nairobi Bw Ali Noor, amesema hospitali za Mogadishu zimeja majeruhi na hazina uwezo wa kuwatibu watu waliojeruhiwa vibaya sana. Awali polisi wa Kenya waliwazuia majeruhi hao pamoja na wabunge kuingia nchini humo wakitoa sababu za kiusalama.

Lakini kibali kilitolewa baada ya Shirika la wakimbizi la Umoja wa Mataifa UNHCR kuingilia kati na kuitaka Kenya kuheshimu sheria za kimataifa za kuwalinda majeruhi wa vita.

XS
SM
MD
LG