Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumatano, Mei 08, 2024 Local time: 08:43

Tshisekedi awateua Bemba na Kamerhe kuwa mawaziri, afanya mabadiliko makubwa katika serikali


Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Felix Tshisekedi
Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Felix Tshisekedi

Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo Felix Tshisekedi amemteua aliyekuwa makamu wa rais wa nchi hiyo Jean-Pierre Bemba, ambaye alikuwa gerezani kwa zaidi ya miaka 10 kwa uhalifu wa kivita, kuwa waziri wa ulinzi wa nchi hiyo katika mabadiliko makubwa kwenye serikali.

Uteuzi wake ulikuwa sehemu ya mabadiliko makubwa ya maafisa 57 wa serikali, ambayo msemaji wa rais alisema ni ya "haraka na lazima", katika tangazo kupitia kituo cha televisheni ya taifa ya Kongo.

Rais huyo pia amemteua Vital Kamerhe, mkuu wake wa zamani wa utawala, ambaye aliachiliwa kutoka gerezani mwezi Desemba 2021 baada ya kupatikana na hatia ya ubadhirifu, wakati alipokuwa waziri wa Fedha. Kamerhe Juni mwaka 2022 alifutiwa mashtaka yote baada ya kukataa rufaa dhidi ya mashtaka hayo.

Mabadiliko hayo, ambayo yalikuwa makubwa zaidi kuliko ilivyotabiriwa, yamekuja kabla ya uchaguzi wa rais uliopangwa kufanyika Desemba 20, ambapo Tshisekedi anatarajiwa kuwania muhula wa pili.

"Huu ni mkanganyiko mkubwa wa kisiasa," alisema Jason Stearns, Mkurugenzi wa Kikundi cha Utafiti cha Kongo na Profesa katika Chuo Kikuu cha Simon Fraser cha Canada.

Uteuzi huo unawaleta vigogo wa kisiasa serikalini, na kuimarisha muungano wa Tshisekedi kuelekea katika uchaguzi, Stearns alisema.

Bemba, kiongozi wa zamani wa waasi alikamatwa mwaka 2008 na Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu wa Kivita kwa uhalifu wa kivita na uhalifu dhidi ya binadamu uliofanywa na wanajeshi wake nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati, kati ya mwaka 2002 na 2003.

XS
SM
MD
LG