Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Mei 03, 2024 Local time: 03:06

Mfalme Charles aeleza masikitiko na huzuni zake kwa waliofanyiwa Wakenya wakati wa kupambana na ukoloni


Mfalme Charles III akipanda mti kwa kushirikiana na Karen Kimani, miaka 10, alipotembelea msitu wa Karura urban wakati wa ziara yake ya kiserikali Kenya huko Nairobi, Nov. 1, 2023.
Mfalme Charles III akipanda mti kwa kushirikiana na Karen Kimani, miaka 10, alipotembelea msitu wa Karura urban wakati wa ziara yake ya kiserikali Kenya huko Nairobi, Nov. 1, 2023.

Mfalme Charles  wa Uingereza amesema amejihisi ana “masikitiko makubwa sana na huzuni” kwa ukatili waliofanyiwa Wakenya wakati wa mapambano yao ya kudai uhuru kutoka wa utawala wa kikoloni wa Uingereza.

Lakini katika hotuba yake mwanzoni mwa ziara yake rasmi ya siku nne nchini Kenya, hakuomba masamaha kamili kama walivyoomba manusura wa ukatili huo na makundi ya kutetea haki ndani ya nchi ambao waliishinikiza serikali ya Uingereza ilipe fidia.

Gideon Mungai bado anakumbuka magumu aliyokabiliana nayo wakati wa mapambano ya kudai uhuru nchini Kenya dhidi ya utawala wa kikoloni wa Kiingereza katikati ya karne ya 20.

Alikuwa mwanaharakati ambaye alifanya kazi na Mau Mau wakati wa uasi wa mwaka 1952 mpaka 1960 katikati mwa Kenya. Kiasi cha wakenya 90,000 waliuawa au kukatwa viungo na takriban 160,000 walitiwa mbaroni, Tume ya Haki za Binadamu ya Kenya – KHRC ilikadiria.

Mungai alizungumza na shirika la habari la Reuters katika siku ya pili ya ziara ya Mfalme Charles wa Uingereza na mke wake Malkia Camilla. Katika dhifa ya kitaifa Jumanne Oktoba 31, Charles alielezea “masikitiko yake makubwa sana” kwa kile alichokiita vitendo vya kuchukiza na visivyo na uhalali vilivyotendwa dhidi ya wakenya wakati wa mapambano yao ya kudai uhuru wa nchi.

Mmoja wa wapigania uhuru akiwa na mavazi ya kiasili amebeba bango wakati wa maandamano kupinga ziara ya Mfalme wa Uingereza Charles III.
Mmoja wa wapigania uhuru akiwa na mavazi ya kiasili amebeba bango wakati wa maandamano kupinga ziara ya Mfalme wa Uingereza Charles III.

Hata hivyo, Mungai na manusura wa manyanyaso ya enzi ya ukoloni walikosoa kushindwa kwake kuomba msamaha kamili au kupendekeza fidia.

“Yeye kusema kuwa wana masikitiko na kutotoa msamaha rasmi inaonyesha wameshindwa kukiri aina ya Ufalme wa Kiingereza na ukoloni ambao umeisababishia nchi hii madhara ya ukoloni ambayo yanaendelea kujitokeza hadi hivi leo katika maisha yetu,” anasema Nicholas Mwangi, Mkaazi wa Nairobi.

Kenya hatimaye ilijipatia uhuru mwaka 1963 na kuwa jamhuri mwaka uliofuata. Jomo Kenyatta, mmoja wa viongozi ambaye alitiwa ndani na Uingereza kwa mapambano ya uhuru, alikuwa rais wa kwanza mpya wa taifa hilo.

FILE - Hayati Jomo Kenyatta
FILE - Hayati Jomo Kenyatta

Uingereza ilifikia makubaliano ya nje ya mahakama na kukubali kulipa fidia ya paundi milioni 20 mwaka 2013, huku wakenya 5,228 walihusika katika kesi hiyo ya pamoja kuhusu manyanyaso yaliyotendwa wakati wa kipindi cha hali ya dharura Kenya mwaka 1952 mpaka 1960.

Malipo, yaliambatana na “taarifa ya majutio” kutoka kwa serikali ya Uingereza, kutokana na kampeni ya miaka 11 na mapambano ya kisheria dhidi ya Uingereza, awali yaliwasilishwa na wazee watano wa Kenya.

Gideon Mungai, mpigania uhuru anaelezea “Kitakachonifurahisha sana katika huu uzee wangu ni kurejeshewa ardhi waliyoipora, huenda siwezi kunufaika na hilo, lakini vizazi vyangu watakuwa na furaha kubwa na mapambano yangu.”

Mwangi Macharia, mkuu wa African Centre for Corrective and Preventive Action, kundi la kutetea haki za binadamu, amesema Uingereza ni vyema ifuate mifano ya Ujerumani, ambayo imeomba msamaha kwa manyanyaso yake nchini Namibia na walikubali kufadhili miradi ya zaidi ya euro bilioni moja.

Wakati Mfalme Charles akipita kwenye mabaki ya ukoloni wa Kiingereza nchini Kenya siku ya Jumanne katika tathmini ya ukatili wa kikoloni kulikuwa na ukatili ambao ulitokea katika nchi jirani ya Tanzania.

Rais wa Ujerumani Frank Walter Steinmeier akiwa katika makumbusho ya maji maji mjini Songea kusini magharibi mwa Tanzania aliomba msamaha kwa vifo vya maelfu ya watu wakati wa uasi wa Maji Maji wa mwaka 1905 mpaka 1907, Steinmeier alisema ujerumani itaendelea kutafuta majibu ya maswali yasiyojibika ambayo hayawapi amani waathirika.

Wataalam wanasema kati ya watu 200,000 mpaka 300,000 walipoteza Maisha wakati wa mapambano hayo.

Habari hii inatokana na mashirika ya habari ya Reuters na AP.

Forum

XS
SM
MD
LG