Trump asema uchunguzi ulioanzishwa dhidi yake ni 'mapinduzi'

Rais Donald Trump

Rais wa Marekani Donald Trump anakosoa uchunguzi ulioanzishwa dhidi yake kumuondoa madarakani na ameuita ni “mapinduzi”, wakati wakuu wa kamati mbalimbali za Baraza la Wawakilishi wamemtuhumu Waziri wa Mambo ya Nje Mike Pompeo kwa hatua yake ya kuzuia juhudi zao za kukusanya nyaraka na kuwahoji mashahidi.

“Kadiri ninavyopata kufahamu mambo mengi zaidi kila siku, ninafikia kuhitimisha kuwa kile kinachofanyika siyo kuniondoa madarakani kisheria bali ni mapinduzi, ya kuwanyang’anya wananchi nguvu zao, kura zao, uhuru wao, haki yao ya kikatiba, uhuru wao wa dini, Jeshi lao, Ukuta wa Mpakani na haki yao waliopewa na Mungu kama Raia wa Marekani” Trump ameandika katika ujumbe wa Twitter.

Wademokrat waliowengi katika Baraza la Wawakilishi wanaendelea na uchunguzi wa kumuondoa rais madarakani ili kuangalia iwapo wanataka kumfungulia mashtaka Trump chini ya amri ya kikatiba inayowalazimisha maafisa wanaojihusisha na “uhaini, rushwa, au jinai nyingine kubwa na makosa mengine kuondolewa madarakani.

Mkaguzi mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje anatarajiwa kukutana Jumatano na wafanyakazi kutoka Baraza la Wawakilishi na kamati mbalimbali za Baraza la Seneti kuzungumzia nyaraka ambazo wabunge wameomba wapatiwe wakati wakichunguza mazungumzo ya simu yaliofanyika Julai kati ya Trump na Rais wa Ukrain Volodymyr Zelenskiy.

Kamati za Usalama, usimamizi na masuala ya kigeni za Baraza la Wawakilishi zilikuwa zimeomba kusikiliza ushahidi utakaotolewa Jumatano kutoka kwa Balozi wa zamani wa Marekani Ukraine Marie Yovanovitch, lakini kikao hicho kilikuwa kimeahirishwa mpaka wiki ijayo. Balozi wa zamani huyo aliyekuwa anaiwakilisha Marekani Ukraine anatarajiwa kuzungumza na kamati hiyo Alhamisi.

Trump amesema hakufanya makosa yoyote katika mazungumzo yake na Zelenskiy. Mtoa taarifa alifungua malalamiko akieleza wasiwasi wake juu ya Trump kuomba nchi ya kigeni kuingilia kati uchaguzi wa mwaka 2020 kwa kuitaka Ukraine kumchunguza mgombea wa chama cha Demokrat Joe Biden.

Pompeo ametuma barua Jumanne kwa Mwenyekiti wa Kamati ya Masuala ya Kigeni ya Baraza la Wawakilishi Eliot Engel akisema maombi ya kupatiwa nyaraka za Wizara ya Mambo ya Nje na ushahidi wa maafisa wa zamani na wa hivi sasa “inaeleweka kama ni jaribio la kuwatishia, kuwanyanyasa na kuwaonea” wafanyakazi wa idara hiyo.

Amesema maombi hayo yanazua “masuala muhimu ya kisheria na utaratibu,” na tahadhari zinazopuuziwa kuwa kutotoa ushirikiano itapelekea kuzuia sheria isifuate mkondo wake.

Engel, katika msimamo ule ule wa Mwenyekiti wa kamati ya usimamizi Elijah Cummings na Mwenyekiti wa kamati ya Usalama Adam Schiff, amejibu kwa kueleza kuwa ripoti zinazoeleza kuwa Pompeo alikuwa ameshiriki katika mazungumzo ya Trump ya simu na Zelenskiy, akisema inamaana bila shaka “anamslahi yanayogongana na kadhia hiyo yaliyowazi” na “hatakiwi kufanya maamuzi juu watakao toa ushahidi au kutoa nyaraka kwani itakuwa analinda maslahi yake na ya Rais.

Wameandika iwapo ni kweli Pompeo ameshiriki katika mazungumzo ya simu, hivi sasa yeye ni “mwenye kutakiwa kutoa ushahidi katika uchunguzi wa kumuondoa rais madarakani.”