Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumanne, Aprili 23, 2024 Local time: 11:34

Ziara ya Lavrov Afrika: Misri inataka Russia kuhakikisha nafaka inafika soko la kimataifa


Waziri wa mambo ya nje wa Russia Sergei Lavrov akiwa katika mkutano na mwenzake wa Misri Sameh Shoukry mjini Cairo, Misri, July 24, 2022. Picha: Reuters
Waziri wa mambo ya nje wa Russia Sergei Lavrov akiwa katika mkutano na mwenzake wa Misri Sameh Shoukry mjini Cairo, Misri, July 24, 2022. Picha: Reuters

Serikali ya Misri imeitaka Russia kutumia mbinu za kisiasa na kidiplomasia kumaliza uvamizi wake nchini Ukraine badala ya kuendelea kuishambulia nchi hiyo kwa mabomu.

Shinkizo hilo limejiri katika kikao kati ya Waziri wa Mambo ya Nje wa Russia Sergey Lavrov na rais wa Misri Abdel Fattah el-Sissi pamoja na viongozi wa umoja wa mataifa ya kiarabu uliofanyika mjini Cairo, wakati Lavrov anaanza ziara yake katika nchi za Afrika, yenye lengo la kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia.

Lavrov, mwanadiplomasia wa ngazi ya juu wa Russia anazitembelea nchi nne za Afrika, kutafuta marafiki wakati nchi yake inaendelea kutengwa na ulimwengu.

Lavrov anatembelea nchi za Afrika ambazo hazikupiga kura kuadhibu Russia

Anazitembeela nchi za Afrika ambazo hazikuunga mkono kura ya Umoja wa Mataifa kuiwekea Russia vikwazo. Anatembelea Misri, Uganda, Jamhuri ya kidemokrasia ya Congo na Ethiopia.

Ziara yake inajiri wakati nchi zote za Afrika zinakumbana na uhaba mkubwa wa nafaka ikiwemo ngano kutokana na uvamizi wa Russia nchini Ukraine.

Serikali ya Misri inaitaka Russia kuchukua hatua za kisiasa na kidiplomasia kumaliza vita hivyo.

"Tumesisitiza kwamba Russia inataka nafaka ifike katika soko la kimataifa.” Amesema Lvrov katika kikao na waandishi wa Habari mjini Cairo. “Tumejadiliana namna tunaweza kushirikiana na mawaziri husika na tumeelewana namna ya kutatua sababu zinazopelekea uhaba wa nafaka.”

Russia imeshambulia bandari ya Ukraine licha ya kusema imeruhusu usafiri wa nafaka

Lavrov amesisitiza kwamba mataifa ya magharibi yamekataa kutilia maanani maslahi ya kiusalama ya Russia kuhusu Ukraine kujiunga na muungano wa NATO, na badala yake kuisikiliza Ukraine kwa kila jambo. Amedai kwamba Ukraine imekuwa inajitayarisha kuanza kutengeneza silaha za biolojia kwamba Marekani ilikuwa na taarifa kuhusu mipango ya Ukraine.

Viongozi wa Misri wanaitaka Russia kuruhusu nafaka kusafirishwa kutoka Ukraine hadi kwenye masoko ya kimataifa.

Russia iliishambulia bandari ya Ukraine ya Odessa, saa chache baada ya nchi hizo mbili kusaini makubaliano ya usafirishaji wa nafaka. Lavrov hajaeleza namna nafaka zitakavyosafirishwa kutoka kwenye bandari za Ukraine iwapo mashambulizi yataendelea.

“Tunataka turudi kwenye mazungumzo kuhusu maswala kadhaa, lakini swala la mazungumzo sio uwamuzi wetu,” amsesema Lavrov, akiongezea “Maafisa wa Ukraine, kutoka kwa rais hadi kwa washauri wake, wamekuwa wakisema kwamba hawataki kufanya mazungumzo hadi pale Ukraine itakaposhinda Russia kivita.”

Russia kukutana na viongozi wa Afrika mwaka ujao, Biden kukutana nao mwishoni mwa mwaka huu

Lavrov amesema kwamba Russia inapanga kuandaa kongamano la viongozi kutoka Afrika katikati mwa mwaka ujao wa 2023 mjini Moscow ili kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia na kiuchumi. Tangazo hilo linajiri siku chache baada ya white house kutangaza kwamba rais Joe Biden atakutana na viongozi wa Afrika mwishoni mwa mwaka huu.

Mwanadiplomasia huyo wa ngazi ya juu wa Russia ameitembelea Misri wiki mbili baada ya rais wa Marekani Joe Biden kutembelea mashariki ya kati, ambapo pia alikutana na viongozi wa Saudi Arabia, Israel, pamoja na kufanya mkutano na viongozi wa umoja wa mataifa ya kiarabu, Misri, Jordan na Iraq, uliofanyika Saudi Arabia.

Wachambuzi wanasema Russia inatafuta marafiki kwa njia zote

Dr. Taha Kizuki ni mhadhiri wa masuala ya Kiafrika katika katika chuo kikuu cha Cairo.

“Tukiangalia ziara ya waziri wa mambo ya nje wa Urusi kwa Afrika ni moja ya ziara ya kuthibitisha yale mahusiano yaliyopo kati ya nchi za Afrika na Urusi na imefanywa ziara kipindi hiki maalumu nahisi ni kama Urusi kuwaambia Waafrika bado tupo pamoja pamoja kwamba na vikwazo tuliowekewa na Ulaya lakini sisi hatuwezi kuwatupa washirika wetu wa Afrika”

Mikataba kati ya Russia na Misri

Misri ni mojawapo ya nchi zinazoagiza kiasi kikubwa cha ngano kutoka Russia na Ukraine. Rais wa Misri El-Sissi alitembelea Serbia wiki iliyopita, ambayo pia ilikataa kuunga mkono vikwazo vya nchi za magharibi dhidi ya Russia. El-Sissi vile vile alitembelea Ujerumani na Ufaransa wiki iliyopita.

Misri na Russia zina mikataba ya kiuchumi na ununuzi wa silaha. Wiki iliyopita, Kampuni ya Russia ya nshati ya Atomiki – Rosatom, ilianza ujenzi wa kinu cha nguvu za atomiki hizo nchini Misri.

Sergei Lavrov atatembelea pia Ethiopia, Uganda, na Congo Brazaville.

Ripoti hii imeandaliwa na Kennes Bwire, VOA, Washington DC akishirikiana na Shaffi Mbinda, VOA, Cairo.

XS
SM
MD
LG