Idadi ya watu ambao wamekufa kutokana na maambukizi ya virusi vya Corona hapa Marekani ilifikia zaidi ya 300,000 Jumatatu, katika siku ambayo chanjo dhidi ya virusi hivyo ilianza kutolewa.
Idadi ya watu ambao wamekufa kutokana na Corona Marekani, ni mara tano zaidi ya idadi ya wamarekani waliokufa katika vita vya Vietnam, na zaidi ya 100 ya idadi ya watu waliokufa katika shambulizi la kigaidi la Septemba 11 mwaka 2001 dhidi ya jengo la kibiashara – world trade center.
Kulingana na hesabu ya chuo kikuu cha Johns Hopkins, zaidi ya watu milioni 16 wameathibitishwa kuambukizwa virusi vya Corona nchini Marekani yenye jumla ya watu milioni 300.
Wahudumu wa afya walikuwa wa kwanza kuanza kupewa chanjo dhidi ya Corona jana jumatatu.
Chanjo inayotolewa Marekani imetengenezwa na kampuni ya Pfizer – BioNTech.
Karibu dozi milioni 3 zimesambazwa kote Marekani, katika zoezi kubwa zaidi la kutoa chanjo kuwahi kufanyika Marekani.
Maafisa wa afya wanasema kwamba watu milioni 20 wanaweza kupata chanjo hiyo kabla ya mwezi huu kumalizika, iwapo chanjo ya pili iliyotengenezwa na kampuni ya Moderna itaidhinishwa katika siku chache zijazo.
Maafisa wa afya wamesema kwamba dozi ya kwanza ya chanjo haitasaidia sana kudhibithi maambukizi.
Imetayarishwa na Kennes Bwire, VOA, Washington DC