Na Mwai Gikonyo, Nairobi
Tatizo la rushwa nchini Kenya limeanza kuchukua sura mpya baada ya shirika la utangazaji la Uingereza-BBC kudai kwamba kiongozi wa upinzani katika Baraza la Senati nchini Kenya, Moses Wetangula, ambaye zamani alikuwa Waziri wa Biashara na Mashauri ya nchi za kigeni alipokea hongo alipokuwa madarakani.
Bwana Wetangula amelifikisha mahakamani shirika hilo la utangazaji BBC kufuatia madai hayo.
Jinamizi la rushwa na hongo nchini Kenya limeanza kuchukua mkondo mpya wa kimataifa nchini Kenya baada ya shirika la BBC kutangaza katika kipindi chake cha Panorama kwamba kiongozi wa upinzani katika Baraza la Senate nchini Kenya, Moses Wetangula alikula hongo baada ya kampuni ya Tumbaku ya BAT kumlipia nauli ya bure ya kusaafiri kutoka Kenya kwenda London.
Bwana Wetangula alikanusha vikali madai hayo na amefungua kesi mahakamani dhidi ya BBC akidai kuchafuliwa jina na sifa ya taaluma yake. Bwana Wetangula aliwakilishwa na kundi kubwa la mawakili.