Netanyahu amesema ameagiza utekelezaji wa sheria hiyo yenye utata usitishwe kwa muda hadi kikao cha bunge cha msimu wa joto ili kutoa fursa kwa ajili ya mazungumzo ya kweli.
Mpango huo unapendekeza bunge liwe na udhibiti mkubwa wa mahakama, ikiwemo uteuzi wa majaji na haki ya kubatilisha maamuzi ambayo bunge haliyataki.
Akitangaza kuahirishwa kwa mpango huo, Netanyahu amesema, “ Kitu kimoja ambacho siko tayari kukubali, kuna watu wachache wenye itikadi kali ambao wako tayari kuisambaratisha nchi, kutupeleka kwenye vita vya wenyewe kwa wenyewe na kutoa wito wa kutohudumu katika jeshi, jambo ambalo ni uhalifu mbaya.”
Kabla ya tangazo la Netanyahu, wafanyakazi wa Israel walianzisha mgomo wa kitaifa Jumatatu, na maelfu ya watu waliandamana tena nje ya bunge.