Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumanne, Aprili 23, 2024 Local time: 14:20

Watu 32 watoweka katika ajali ya meli China


Meli ya mafuta ya kampuni ya Sanchi ikiwaka moto katika pwani ya mashariki ya China.
Meli ya mafuta ya kampuni ya Sanchi ikiwaka moto katika pwani ya mashariki ya China.

Watu 32 ambao hawajulikani waliko wanatafutwa baada ya meli ya mafuta na meli ya mizigo kugongana nje kidogo ya pwani ya mashariki ya China Jumamosi jioni.

Meli ya mafuta ya kampuni ya Sanchi, iliyosajiliwa Panama ilikuwa imebeba tani 136,000 za mafuta kutoka Iran ilishika moto baada ya kugongana.

Meli ya mizigo iliyokuwa imesajiliwa Hong Kong, CF Crystal, ilikuwa imebeba tani 64,000 za nafaka kutoka Marekani zikielekea jimbo la Guangdong upande wa kaskazini wa China. Wafanyakazi wake wote waliookolewa ni raia wa China, wizara ya usafiri ya nchi hiyo imeeleza.

Wizara ya Usafirishaji ya China imesema watu waliotoweka katika ajali hiyo ni wafanyakazi wa meli hiyo 30 wananchi wa Iran na raia wawili wa Bangladeshi.

Wafanyakazi 21 wakakamavu wa meli ya mizigo wameokolewa, wizara hiyo imesema.

“Meli hiyo ya Sanchi bado inaendelea kuwaka moto huku ikielea mpaka sasa. Kuna mabaki ya mafuta yanaelea baada ya mlipuko huo na tunaendelea na juhudi za ukoaji,” wizara imesema.

Ajali hiyo imetokea eneo ambalo ni maili 296 kutoka pwani ya Shanghai.

Meli nane za China zimepelekwa katika eneo hilo kwa ajili ya kuwatafuta waliotoweka baada ya ajali hiyo na shughuli za uokoaji, Shirika la habari la China Xinhua limesema.

Korea Kusini pia imepeleka meli yake ya kivita na helikopta kusaidia juhudi za uokoaji.

Meli hiyo ya mafuta ilikuwa inaelekea eneo la Daesan, Korea Kusini kutoka Kisiwa cha Kharg, Iran, kwa mujibu wa takwimu za usafirishaji wa meli za shirika la Reuters.

Ilikuwa imebeba shehena ya thamani ya Dola za Kimarekani milioni 60 ambayo ni chini kidogo ya mapipa ya mafuta milioni moja.

XS
SM
MD
LG