Maafisa wamewahamisha mamia ya watu wanaotafuta hifadhi kutoka kwenye kambi ya muda nje ya kituo cha kupokea wahamiaji chenye msongamano kaskazini mashariki mwa Uholanzi.
Hatua hiyo imekuja baada ya ripoti moja mbaya kutaja eneo ambalo takriban watu 700 walikuwa wakilala vibaya wiki hii na ni hatari ya kiafya. Timu ya Ukaguzi wa Huduma za Afya na Vijana ilisema baada ya kutembelea kambi hiyo ya muda nje ya kituo katika kijiji cha Ter Apel kwamba kulikuwa na "hatari kubwa ya milipuko wa magonjwa ya kuambukiza kwa sababu ya ukosefu mkubwa wa usafi."
Msemaji wa shirika la serikali la watafuta hifadhi alisema leo Jumamosi kwamba karibu watu 400 wanaotafuta hifadhi walihamishwa usiku kucha hadi kwenye makazi mbadala katika manispaa tofauti.