Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Machi 29, 2024 Local time: 13:16

Wanawake Sudan Kusini washinikiza rais kuchukua hatua


Wanawake wa Sudan Kusini wakidai haki zao na amani wakati wa maandamano mjini Juba, Julai 13, 2018.
Wanawake wa Sudan Kusini wakidai haki zao na amani wakati wa maandamano mjini Juba, Julai 13, 2018.

Viongozi wa wanawake wa Sudan Kusini wamemtaka rais wa nchi hiyo kutenga asilimia 35 ya uteuzi katika nafasi za kiutendaji kwa ajili ya wanawake, kama ilivyo kubaliwa katika makubaliano ya amani ya karibuni.

Hivi karibuni, Rais Salva Kiir amewateua watu 10 kuunda kamati iliyopewa jukumu la kuanzisha utaratibu wa kuunda serikali ya mpito ya Sudan Kusini. Ni mwanamke mmoja tu aliye teuliwa katika kamati hiyo ya watu 10.

Mary Ayen Majok, Mbunge wa Bunge la mpito, ameiambia VOA siku ya Jumatano kwamba haja furahishwa kwani mgao kwa upande wa wanawake haujafikiwa.

“Hatua ya kuteua asilimia 35 ya uwakilishi wa wanawake haija tekelezwa,” amesema Majok. “Kwetu sisi, kwa kweli tunahisi vibaya kwa sababu ina maana kwamba pande husika hazina nia ya dhati ya kutimiza kile walicho kubaliana.”

Regina Joseph Kaba ambaye anawakilisha kundi la zamani la Sudan People’s Liberation Movement Political Detainees (FDS), moja ya vyama ambavyo vimetia saini makubaliano ya amani huko Addis Ababa, Ethiopia, anasema uwiano wa jinsia ni mapambano yanayoendelea na kuongezea kwamba mchanganyiko katika kamati ya NPTC haujafuata misingi ya makubaliano ya Addis.

“Wamekiuka asilimia ya uwakilishi wa wanawake.Tulitakia kuwa na walau wanawake wawili katika kamati ya NPTC,” amesema Kaba.

Makubaliano ya Addis siyo tu yametenga asilimia 35 ya nafasi za utendaji kwa ajili ya wanawake, pia ulijumuisha mpango mpana kwa pande zote kufikiria kwa kiasi kikubwa suala la ukabila, jinsia na uwakilishi wa kieneo.

Emily Koiti ambaye aliwakilisha vijana wa Sudan Kusini katika mashauriano ya amani ambayo yalikamilika hivi karibuni, amesema pande zote katika makubaliano hayo zilizungumzia kiini cha mzozo wa Sudan Kusini kama wana nia ya dhati katika utekelezaji wa makubaliano hayo.

“tunataka kuhakikisha kwamba kuna uwakilishi wa kieneo, kikabila na kizazi katika taasisi zote ambazo zitaundwa kulingana na makubaliano yaliyo fikiwa,” Koiti amesisitiza.

Ukiukaji wa Sitisho la Mapigano

Chris Trot, mwakilishi maalum wa Uingereza kwa Sudan na Sudan Kusini ameiambia VOA wiki iliyopita kwamba pande zilizohusika katika mzozo wa Sudan Kusini zina fursa ya kuonyesha nia yao ya dhati katika utekelezaji wa kufufua mkataba wa amani uliotiwa saini Septemba 12.

Siku chache tu baada ya kutiwa saini kwa mkataba, ripoti za mapigano ziliibuka katika sehemu kadhaa za Sudan Kusini, kwa mujibu wa Jean-Pierre Lacroix, katibu mkuu msaidizi wa Umoja wa Mataifa.

Angelia Teny, mwanachama mwandamizi wa kundi la uasi la Sudan Peoples Liberation Movement in Opposition (SPLM-IO), ameyalaumu majeshi ya serikali kwa kushambulia ngome za uasi katika eneo la Central Equatoria na lililo kuwa jimbo la Unity.

“Tuliliwasilisha suala hili na wapatanishi wetu katika makubaliano ya amani, tumeliwasilisha kwa rais,” Teny amesema. Amesema serikali inajitahidi kuweka makamishna katika maeneo ambayo yako chini ya udhibiti wa waasi.

Lam Tungwar, Waziri wa Habari katika jimbo la Liech, ambalo awali lilikuwa ni jimbo la Unity amesema wapiganaji wa kundi kuu la uasi la SPLM-IO wanaomtii makamu rais wa zamani Riek Machar wameshambulia maeneo ya serikali katika kijiji kidogo katika kaunti ya Koch wiki hii.

Taasisi ya Cease-Fire transitional Security Arrangement Monitoring Mechanism (CTSAMM) ambayo inafuatilia ukiukaji wowote wa sitisho la mapigano, imeiambia VOA katika ujumbe wake wa barua pepep kwamba “hivi sasa wanachunguza ukiukaji wa sitisho la mapigano katika eneo la Yea. Uchunguzi unaendelea na itakuwa si muafaka kuzungumzia suala hili kwa wakati huu.”

XS
SM
MD
LG