Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Aprili 25, 2024 Local time: 12:14

Makundi hasimu Sudan Kusini yasaini mkataba wa serikali ya kitaifa


Rais wa Sudan Kusini Salva Kiir asaini mkataba wa serikali ya kitaifa uliozileta pamoja pande hasimu nchini humo, Agosti 5 2018, in Khartoum.
Rais wa Sudan Kusini Salva Kiir asaini mkataba wa serikali ya kitaifa uliozileta pamoja pande hasimu nchini humo, Agosti 5 2018, in Khartoum.

Makundi yanayo hasimiana nchini Sudan Kusini yamesaini mkataba wa amani unaounda serikali ya kitaifa Jumapili, katika juhudi za kumaliza vita vya wenyewe kwa wenyewe vilivyodumu kwa miaka 5 na kusababisha vifo vya maelfu ya watu na mamilioni kukimbilia nchi jirani.

Kwa mujibu wa shirika la habari la Sudan, SUNA, Rais wa Sudan Kusini Salva Kiir na kiingozi wa waasi, aliyekuwa makamu wake Riek Machar wamesaini mkataba wa amani katika mjii wa Khartoum, Sudan.

Muundo mpya wa serikali

Chini ya mkataba huo, Salva kiir atasalia kuwa rais, na Riek Machar kurudi nyumbani na kuwa makamu wa rais wa kwanza, huku nafasi tano za makamu wa rais zikiundwa.

Kutakuwepo serikali ya mpito ya miezi 8 itakayoongozwa na Salva Kiir, na baadaye serikali ya mpito ya miaka 3.

Kutokana na mkataba huo, serikali itakuwa na mawaziri 20 kutoka kwa chama cha Kiir, tisa kutoka chama cha Machar na sita kutoka makundi mengine.

Hii ndio hatua ya hivi karibuni kati ya hatua kadhaa zilizowahi kuchukuliwa kuleta amani nchini Sudan kusini tangu mwaka wa 2013.

Mkataba wa amani wa 2016

Mkataba wa amani ulivunjika July 2016 wakati mapigano yalipozuka katika mji wa Juba na kupelekea Machar kutoroka nchini kwa kupitia njia za vichakani.

Tangu mda huo, amekuwa chini ya kifungo cha nyumbani nchini Afrika kusini.

Serikali ya Sudan Kusini inasisitiza kwamba mara hii, mambo yatakuwa tofauti kati ya viongozi hao wawili na kwamba Machar amejifunza "kupitia hali ngumu" na kwamba ameahidi kushirikiana na Kiir kwa sababu hataki kurudi nchini Afrika kusini.

Katika kikao na waandishi wa habari, msemaji wa serikali ya Sudan kusini Michael Makuei amesema kwamba wapiganaji wa Salva Kiir watapewa mafunzo na kujiunga na jeshi la taifa.

Mkataba huo ni hatari?

Mchambuzi wa siasa za Sudan Kusini Alan Boswell ametaja mkataba huo kuwa hatari.

"Mnamo mwaka 2013, Riek alitaka kuchukua nafasi ya Kiir lakini Kiir alijibu kwa nguvu zote na kumfukuza serikalini. Mwaka 2016, hali ilikuwa hivyo hivyo. Matokeo hayo mawili yalisababisha vita vikubwa. Mkataba huu wa amani, unaeka mazingira yale yale ya mwaka 2013 na 2016," amesema Allan akiongezea kwamba "mkataba unapovunjika, unavunjika vibaya sana".

Mikataba ya amani umesainiwa katika siku za hivi karibuni lakini imevunjika ndani ya masaa machache baada ya kusainiwa.

Jumuiya ya Kimataifa

Uvumilivu wa jumuiya ya kimataifa umekuwa ukitoweka, Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa likiiwekea Sudan Kusini vikwazo vya silaha.

Mnamo mwezi July, bunge la Sudan Kusini liliongeza muda wa serikali hadi mwaka 2021, hatua ambayo iliwakasirisha wanasiasa wa upinzani waliosema kwamba serikali ilikuwa katika mchezo kwenye meza ya mazungumzo ya kuleta amani ya kudumu.

Raia wa Sudan Kusini

Raia wa Sudan Kusini wanasema kwamba wamechoka na maisha ya vita na wanataka hali ya utulivu.

"Kwa kweli tunataka amani kwa sababu tumechoka na vita" amesema Santino Deng, mkaazi wa mji wa Juba.

Hata hivyo baadhi ya makundi ya kutetea haki za kibinadamu yamesifia mkataba wa amani uliofiikiwa hivi sasa, lakini yakaonya kwamba ni hatua ya mwanzo tu.

" Ili kuzuia vita kuzuka tena, mkataba huo unastahili kuhakikisha kwamba mamlaka mengi hayasalii katika mikono ya watu wachache," amesema Brian Adeba, naibu wa mkurugenzi wa shirika la sera - enough project- lenye makao makuu jijini Washington.

XS
SM
MD
LG