Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumanne, Machi 19, 2024 Local time: 08:36

Wanafunzi 20,000 waacha kuhudhuria masomo Burundi


Wanafunzi zaidi ya elfu 20 waliokuwa wanapatiwa chakula shuleni na shirika moja la Kijerumani lisilo kuwa la kiserikali katika mkoa wa Kirundo kaskazini mwa Burundi wameacha kuhudhuria masomo shuleni.

Wakiongea na Sauti ya Amerika viongozi wa elimu katika mkoa huo wamesema wanafunzi laki moja na nusu wa shule za msingi katika mkoa huo, walikuwa wanapatiwa msaada wa chakula kutoka shirika hilo, kwa kupata mlo shuleni ili wasiache shule baada ya kudhihirka kwamba familia zao zinakabiliwa na umaskini.

Hiyo ni moja ya athari ya hatua ya serikali ya Burundi kusitisha shughuli za mashirika yasiyo ya kiserikali (NGOs ) 130 tangu tarehe mosi Oktoba, kwa madai kuwa mashirika hayo ya hisani hayaheshimu sheria mpya inayoongoza shughuli za mashirika ya kimataifa ya kigeni.

Serikali ilitowa masharti kadha kwa mashirika hayo na kuyapa muda wa miezi mitatu ili yawe yamekwisha tekeleza masharti hayo ili yaweze kuendele kufanya kazi.

Baadhi ya masharti hayo, ni pamoja na mashirika hayo ya kigeni kuweka pesa zao zote za matumzi za kigeni kwenye benki kuu ya taifa na kuhakikisha usawa kati ya makabila muhimu ya Burundi wakati wa kuajiri wafanyakazi.

Wakati hayo yakijiri, wawakilishi wa nchi zinazofadhili NGOs hizo ambazo ni Marekani, Canada, Japan, USwiss, Umoja wa Ulaya na Shirika la Umoja wa Mataifa linalo simamia maendeleo (UNDP), wametowa tamko kwa vyombo vya habari wakiomba kuwepo mazungumzo zaidi na Serikali ya Burundi, ili kupata mwanga na muwafaka kuhusu masharti yaliotolewa.

Katika tamko hilo, wawakilishi wa nchi hizo wamesema, “ tunaelewa matakwa ya serikali ya Burundi, lakini na sisi tunaomba serikali kuelewa maadili na utaratibu wa nchi zinazofadhili mashirika ya kimataifa ya hisani.”

Imetayarishwa na Mwandishi wetu Patrick Nduwimana, Washington, DC

XS
SM
MD
LG