Waislam kote duniani wanasherehekea siku kuu ya Eid el-Fitr, siku inayoadhimisha kuhitimishwa kwa mwezi mutukufu wa Ramadhan.
Nchini Uganda waislam walisherehekea siku hiyo kwa kuwaombea waislam wenzao wa Libya wakati nchi hiyo inapokabiliwa na vita na mzozo mkubwa wa kisiasa. Katika Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo, waislam pia walisherehekea siku hiyo Jumanne huku viongozi wa kidini wakitoa mwito kuwe na utulivu wa kisiasa na uchaguzi huru na wa haki wakati wa uchaguzi ujao Novemba mwaka huu.
Waislam wengi nchini humo walisema mwezi huo umekuwa wa shida kubwa kutokana na ongezeko la bidhaa za kimsingi hususan chakula. Nchini Kenya ni baadhi tu ya waislam waliosherehekea siku kuu hiyo Jumanne huku maelfu ya wengine wakipanga kuisherehekea Jumatano.
Waislam kutoka Misri, Syria na nchi kadha za kiarabu pia walisherehekea Eid el-Fitr Jumanne kwa sala katika misikiti mbalimbali katika nchi zao. Nchi nyingine zisizo za kiarabu ambapo waislam walisherehekea siku kuu hiyo Jumanne ni pamoja na Russia, Uturuki na Afghanistan
Lakini katika taifa la Indonesia lenye waumini wengi zaidi wa dini ya Kiislam duniani, sherehe za Eid el-Fitr zitafanyika Jumatano Agosti 31.