Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Aprili 19, 2024 Local time: 16:50

Wahudumu wa afya wa kimataifa wakutana Kenya kujadili mtaala wa tiba


Rais Uhuru Kenyatta
Rais Uhuru Kenyatta

Wahudumu wa afya kutoka mataifa 99 ulimwenguni wamekutana Jumatatu Mombasa, Kenya kujadili mtaala wa pamoja kwenye nyanja ya utabibu.

Mkutano huo ambao utamalizika Jumatano ni wa kwanza wa aina yake unalenga kushughulikia mtaala wa elimu kwa wahudumu wa afya na jinsi ya kutumia teknolojia ya kisasa kuimarisha utoaji huduma kufikia viwango vya kimataifa.

Maafisa wa afya wanaohudumu katika vituo vya afya kibinafsi, vinavyomilikiwa na mashirika yasio ya kiserikali pamoja na vile chini ya taasisi za kidini wanajadiliana jinsi ya kuendelea kutoa huduma baada ya janga la Covid pamoja na utoaji huduma chini ya mpango wa afya kwa wote.

Mapendekezo kutoka mkutano huu yatatumika kurekebisha sera za utoaji huduma za kiafya, utoaji elimu kwa wahudumu wa afya wakihusisha teknolojia ya kisasa.

Akifungua kongamano hilo Rais Uhuru Kenyatta amewahimiza wahudumu hao kubuni mapendekezo yatakayorekebisha, kubadilisha na kuimarisha hali ya utoaji huduma za kiafya kote ulimwenguni.

Amesema kuwa serikali yake imetekeleza sera kadhaa kuimarisha utoaji huduma za afya nchini Kenya ikiwemo kutekeleza mpango wa hazina ya bima ya kitaifa ya malipo ya hospitalini kwa wote.

Ameeleza takriban watu milioni 1.2 wanaoishi na virusi vya HIV wanahudumiwa na bima hiyo ya kitaifa kwa wote, wanawake wajawazito pamoja na wale wanaotibiwa kifua kikuu, TB.

Waziri wa Elimu Kenya George Magoha amesisitiza umuhimu wa kuainisha elimu ya utabibu kwenye mfumo wa mpya wa elimu, CBC, ili kuchochea hamu ya kusomea utabibu kwa wanafunzi.

Baada ya mkutano huo Rais Uhuru Kenyatta alizindua rasmi mpango wa kitaifa wa kutoa huduma za afya kwa wote.

Washiriki kutoka mataifa 24 ikiwemo watafiti wataalamu kutoka China, Korea Kusini na kadhalika wako Mombasa kwa kongamano hilo huku wengine wakilifuatilia mtandaoni.

XS
SM
MD
LG