Rais Joe Biden akizungumza Jumapili wakati wa sherehe za kitaifa kutoa heshima kwa maafisa wa polisi waliouliwa wakiwa kazini, alianza hotuba yake kwa kuzungumzia shambulio hilo la Buffalo.
Amesema anapokea habari zote na wizara ya sheria inafanya uchunguzi wa tukio hilo kama uhalifu wa chuki na kutoa wito kwa wamarekani kusimama pamoja dhidi ya chuki.
Kijana mzungu mwenye umri wa miaka 18, anayetuhumiwa na shambulio hilo, amefunguliwa mashtaka Jumamosi jioni baada ya kuwauwa watu 10 na kuwajeruhi wengine watatu katika duka la chakula la Tops, kwenye mtaa wa watu weusi mjini Baffalo, New York.
Maafisa wa usalama wanasema mtuhumiwa aliyekuwa na bunduki kubwa na ikionekana ametenda uhalifu huo pekee yake alisafiri kwa gari lake kutoka nyumbani kwake wilayani New York, saa chache kutoka mahali alipotenda mauaji ambayo amerikodi na kutangaza kwenye ukurasa wake wa mtandao.
Polisi wanasema watu 11 kati ya 13 walioshambuliwa walikuwa ni watu weusi.
Hati za mahakama zinamtaja kama Payton Gendron kutoka mji wa Conklin, mji wenye wakazi elfu 5, karibu na mpaka wa Pennsylvania.
Mwendesha mashtaka wa wilaya, Erie John Flyn anasema amefunguliwa mashtaka ya mauaji saa chache baada ya kukamatwa katika mahakama ya jimbo, mashtaka ambayo yataweza kumpatia kifungo cha juu cha maisha jela.
Meya wa Buffalo, Byron Brown amesema hii ni siku ya huzuni mkubwa kwa wakazi wa mji wake akitoa wito kwa serikali kuu kukomesha hotuba za chuki na chuki kwenye mitandao pamoja na kupitishwa sheria za kubana umilikaji bunduki Marekani.