Maelezo hayo yanafuatiwa na mkutano wa ujumbe wa ECOWAS, ambao umetumwa kukutana na uongozi wa kijeshi ambao umechukua madaraka wiki iliyopita, yakiwa mapinduzi ya pili kukumba taifa hilo la afrika magharibi mwaka huu.
Traore amesema Burkina Faso itaheshimu makubaliano yaliyofikiwa na ECOWAS mwezi Julai, ya kurejesha utawala wa kikatiba ndani ya miezi 24. Amesema pia kwamba utawala wake utaheshimu nia ya dhati ya kimataifa hasa katika kulinda haki za binadamu pamoja na kushirikiana na jopo la tathimni ya Ecowas.
Mpatanishi wa Ecowas anayeongoza ujumbe huo, rais wa zamani wa Niger Mahamadou Issoufou Jumanne alisema ameridhika na mabadilishano hayo. Traore ameongoza mapinduzi yaliyomuondoa madarakani kiongozi wa kijeshi Paul Henri Damiba, aliyechukua madaraka katika mapinduzi ya awali mwezi Januari, na kuiahidi ECOWAS kurejesha utawala wa kiraia ifikapo Julai 2024.