Daftari la kumbukumbu ya vitambulisho inaonyesha kati ya vitambulisho 128,926 Tume ya Uchaguzi imegundua kuna vitambulisho 107,777 vilikuwa na namba moja lakini majina tofauti.
Uchambuzi zaidi unaonyesha kuwa vitambulisho 53,671 vimetolewa zaidi ya mara moja.
Wakati mchakato wa kuwasajili wakenya kupiga kura ukiingia siku yake ya tisa Jumanne, mgogoro kuhusu usajili huo umeanza kujitokeza.
Lakini Tume ya Uchaguzi chini ya usimamizi wa mwenyekiti wake mpya, Wafula Chebukati Jumanne imeeleza kuwa tayari imeshapata ufumbuzi juu ya tatizo hili na imeonya wakenya kuacha mara moja kujisajili zaidiya mara moja.
Hata hivyo, Chebukati ametoa onyo kali kwa wakenya watakaopatikana kufanya kusudi kujisajili maradufu na watachukuliwa hatua za kisheria.
Mwandishi wa Idhaa ya Kiswahili VOA ameripoti kuwa baadhi ya hila za wanasiasa zimeanza kujitokeza.
Vinara wa upinzani Raila Odinga na Kalonzo Musyoka wamekuwa wakieleza kuwa vitambulisho vyao vimetumika kuwasajili watu wengine katika maeneo mbalimbali.
Mwandishi wetu amesema hali hii imeendelea kuzua utata mkubwa wa kisiasa kwa hofu ya kuzuka suintofahum.
Madai kuwa maelfu ya wakenya wamejisajili mara mbili pia yamejitokeza wazi.
Lakini lile ambalo limekuwa likileta mtafaruku wa kisiasa ni jinsi vitambulisho vya vinara wa upinzani Raila Odinga na Kalonzo Musyoka vilivyotumika kuwasajili watu tofauti katika maeneo mengine.
Wanasiasa hao tayari wameeleza wasiwasi wao kuwa huenda pana hila ya kisiasa itakayotumika kuhujumu zoezi zima na hata matayarisho ya uchaguzi mkuu.
Katika wiki moja ya usajili huo tayari watu 825,145 wamejisajili kuwa wapiga kura ikiwa ni asilimia 58 kati ya watu milioni 1.4 wanaolengwa kusajiliwa.
Imetayarishwa na mwandishi wetu Kennedy Wandera, Kenya