Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Machi 28, 2024 Local time: 22:30

Uchaguzi Comoros: Upinzani wakataa matokeo yanayotarajiwa


Rais wa Comoros Azali Assoumani
Rais wa Comoros Azali Assoumani

Vituo vya kupigia kura vilifungwa Jumapili jioni katika visiwa vya Comoros kufuatia uchaguzi uliozua utata ambapo rais wa sasa Azali Assoumani anatarajiwa kutangazwa mshindi licha ya wapinzani wake kudai kwamba uchaguzi huo uligubikwa na dosari nyingi.

Upinzani unadai kwamba uchaguzi huo wa urais uligubikwa na udanganyifu ikiwa ni pamoja na kuwazuia waangalizi huru kufuatilia yaliyokuwa yanaendelea katika vituo mbalimbali.

Aidha viongozi wa upinzani wametoa wanadai kwamba maafisa wa tume ya uchaguzi, CENI, walipatika wakijaza karatasi za kupigia kura hata kabla ya zoezi hilo kufunguliwa rasmi.

Baadhi ya wakazi wa mji mkuu Moroni wamenukuliwa na shirika la habari la AFP wakisema kwamba walishuhudia makabiliano kati ya wapiga kura na polisi huku wengine wakisema zoezi la upigaji kura liliendelea kwa amani katika maeneo mbalimbali ya visiwa hivyo vidogo.

Wagombea wa upinzani wamesema baadhi ya wafuasi wao walikamatwa na polisi na kuongeza kuwa dosari zilizoripotiwa katika vituo mbalimbali na tume ya uchaguzi "ni sawa na jaribio la mapinduzi."

Lakini mkurugenzi wa kampeni ya rais Assoumani amepuzilia mbali madai hayo. Akizungumza na shirika la habari la AFP Jumapili, Houmed Msaidia, amesema uchaguzi huo ulikuwa wa haki na kweli na upinzani unataka kuzua taharuki bila sababu halali.

Msaidie amesema wanaodai kuwa uchaguzi huo haukuwa wa haki wako huru kutumia njia za kisheria kuwasilisha malalamishi yao.

Takriban watu laki tatu walipiga kura katika visiwa hivyo ambavyo vina jumla ya wakazi laki nane.

Wagombea 13 walikuwa wamejiandikisha kuwania nafasi hiyo ya urais na matokeo rasmi yanatarajiwa kutangazwa Jumatatu.

XS
SM
MD
LG