Idara ya Umoja wa Mataifa ya kuhudumia wakimbizi inaitaka serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo-DRC kuhakikisha ulinzi kwa wakimbizi na wanaoomba hifadhi baada ya wanajeshi wa Congo kuwafyatulia risasi na kuwauwa waandamanaji wasiopungua 39 wa Kirundi akiwemo mtoto mmoja.
Kwa mujibu wa shirika la habari la Associated Press-AP idara hiyo ilisema Jumanne kwamba watu wengi waliokufa pamoja na watu 94 waliojeruhiwa walikuwa wakimbizi pamoja na wanaotafuta hifadhi.
Maafisa wa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo wanasema wameanzisha uchunguzi kuhusiana na ufyatuaji risasi uliotokea Ijumaa ambapo idara ya wakimbizi inasema watu hao walianza maandamano ya amani kufuatia kukamatwa kwa baadhi ya warundi ambao walikhofia kufukuzwa nchini humo.
Mkuu wa idara ya wakimbizi katika Umoja wa Mataifa, Filippo Grandi anasema tukio hilo baya halikutakiwa kutokea na anaitaka serikali ya Congo kuanzisha uchunguzi wa kina. Idara ya Umoja wa Mataifa inasema hali huko Kamanyola mashariki mwa Congo bado ni tete na zaidi ya warundi 2,400 wanatafuta hifadhi karibu na kambi ya walinda amani wa Umoja wa Mataifa.