Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Julai 27, 2024 Local time: 04:10

UN : Watu zaidi ya milioni 11 wakabiliwa na ukosefu wa chakula kusini mwa Afrika


Mmiliki wa mifugo ya kondoo Gertruida Buffel
Mmiliki wa mifugo ya kondoo Gertruida Buffel

Wakulima wameshuhudia ukame mbaya sana uliowahi kuonekana kwa miongo kadhaa.

Ukame huo unaathiri sehemu kubwa ya kusini mwa Afrika. Wakulima wengi wanajitahidi kuhakikisha watu na mifugo inaendelea kuwa hai, wakati Umoja wa Mataifa (UN) ukionya kwamba zaidi ya watu milioni 11 hivi sasa wanakabiliwa na mgogoro mkubwa wa ukosefu wa chakula.

Miezi kadhaa ya ukame imeliathiri eneo kubwa la kusini mwa Afrika. Kwa mujibu wa shirika la mpango wa chakula duniani, WFP, eneo la kusini mwa Afrika limepata mvua za kawaida mara moja tu katika muda wa misimu mitano ya upandaji mazao.

Wakati huohuo wakulima wadogo wadogo ndiyo walioathiriwa vibaya sana na ukame. Mmiliki mmoja wa kondoo aliyekufa, Gertruida Buffel, mwenye umri wa miaka 55, ameamua kugawana chakula chake na wanyama anaowafuga.

Kwa wiki mbili amewapatia chakula kondoo wake wawili wadogo kwa kuwapa mchanganyiko wa unga wa mahindi na maji baada ya mama yao kufariki kwa njaa. Ni hivi punde amerejea nyumbani na kubaini kuwa kondoo wake alishindwa kustahmili njaa iliyokuwa inamkabili.

“Niliporejea nyumbani, nilimkuta kondoo wangu mmoja amekufa. Nilimuona usiku uliopita, na alikuwa katika hali ambayo si nzuri kiafya, na alikuwa hawezi kula mchanganyiko wa unga wa mahindi aliokuwa anapewa. Hivi sasa, sina uhakika kama ni kwasababu sisi tunamlisha unga wa mahindi, lakini nilimuona kwa macho yangu kuwa hali yake ni mbaya,” anasema Gertruda Buffel mkazi wa Vosburg.

UN unakadiria kwamba zaidi ya watu milioni 11 wanakabiliwa na viwango vya juu vya mgogoro wa ukosefu wa usalama wa chakula katika maeneo kama vile Zimbabwe na Msumbiji, ambao vimbunga viwili vimesafisha kabisa mazao yote mapema mwaka huu.

Wakulima wengi katika jimbo la Northern Cape nchini Afrika Kusini, ni miongoni mwa maeneo yaliyoathiriwa vibaya, na juhudi zinafanyika kuhakikisha watu na mifugo wanaishi wakati mapato yakiwa yameanguka na madeni yameongezeka.

Mkulima wa mifugo ya kondoo wa biashara, Louis Van Der Mere, mwenye umri wa miaka 64, amelia wakati anaelezea kupoteza zaidi ya kondoo 400 na mifugo mingine 450 katika muda wa miaka miwili iliyopita kwa sababu ya ukame mbaya sana ambao hajawahi kuuona kwa kipindi cha miaka 45 ya kilimo.

“Hali ni ngumu sana huko Kienomerkie, tunahisia kubwa. Nimepoteza asilimia 25 ya kondoo wetu. Mifugo mingine nayo pia inanipatia kipato, tunawauzia baadhi ya watu wanaokuja kwenye shamba langu. Nilikuwa na mifugo kati ya 450 na 500, siwezi kupata chochote zaidi ya kuangalia mifugo iliyokufa,” Louis van der Merwe, mkulima wa kondoo.

Kasisi Jaco Heymans wa kanisa la Dutch Reformed amekuwa akitoa ushauri nasaha kwa wakulima wengi na wafanyakazi wa kwenye mashamba huko Vorsburg.

“Watu wengi wanajitahidi sana kuachana na mawazo ya kujiua kwa wakati huu hapa na huko sehemu za magharibi, kwa sababu ukame umeathiri sehemu kubwa ya Afrika Kusini. Sidhani watu wanafahamu ukubwa wa tatizo lakini kimsingi sehemu yote katika katikati mwa nchi hapa Afrika Kusini ina ukame,” anasema Jaco Heymans kasisi wa kanisa la Dutch Reformed.

Mashamba makubwa ya biashara yanashirikiana chakula chao na wakulima wadogo wadogo, na kanisa linatoa ushauri nasaha kwa kila mtu kuanzia wamiliki wa mashamba mpaka vibarua ambao wanakhofia kupoteza ajira zao. Watabiri wa hali ya katika idara hiyo nchini Afrika Kusini wanasema wanatabiri kuwa mvua zitakazonyesha zitakuwa chini ya viwango vya kawaida nchini humo na kote katika eneo zima la kusini mwa Afrika katika muda wa miezi mitatu ijayo.

Imetayarishwa na mwandishi wetu, Khadija Riyami, Washington, DC

XS
SM
MD
LG