Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Aprili 25, 2024 Local time: 02:07

Umoja wa Mataifa waongeza muda wa ujumbe wake Libya kwa miaka mitatu


Waziri Mkuu wa Libya Abdulhamid al-Dbeibah.
Waziri Mkuu wa Libya Abdulhamid al-Dbeibah.

Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa limeongeza  muda wa ujumbe wake wa kisiasa nchini Libya kwa muda wa miezi mitatu.

Baraza hilo lilipiga kura kwa kauli moja Ijumaa huku Marekani na Uingereza zikiishutumu Russia kwa kuzuia kuongezwa kwa mamlaka ya muda mrefu na madhubuti zaidi, ambayo yangejumuisha kuendeleza mchakato wa maridhiano ya pande zinzozozana, ambazo kwa sasa kila upande unadai kwamba ndio unaoongoza.

Kwa mujibu wa shirika la habari la Associated Press, AP, Balozi wa Russia katika Umoja wa Mataifa, Vassily Nebenzia, aliema nchi yake inasisitiza kuongezwa muda wa miezi mitatu ili kumshinikiza Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres kumteua haraka mwakilishi mpya atakayeuongoza ujumbe maalum wa Umoja wa Mataifa nchini Libya, maarufu UNSMIL.

Gabon, Ghana na Kenya, nchi tatu za Afrika ambazo ni wanachama wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa zimezitolea wito pande zinazohasimiana nchini Libya, kuweka kando tofauti zao za kisiasa na kuongeza kwamba njia za kijeshi hazitaleta suluhisho endelevu la Amani.

Nchi hizo zimelaani uingiliaji wa kijeshi nchini Libya, na zimetaka kuondoka kwa wapiganaji wote wa kijeshi na mamluki na zimeutaka Umoja wa Mataifa, Umoja wa Afrika na washirika wa kimataifa kuunga mkono mazungumzo ya kitaifa na maridhiano nchini Libya.

Libya, taifa la Afrika Kaskazini lenye utajiri mkubwa wa mafuta lilitumbukia katika hali ya machafuko tangu vuguvugu la mapinduzi lililoungwa mkono na Jumuia ya Kujihami ya NATO na kumuondoa madarakani kiongozi wa muda mrefu Muammar Gaddafi mwaka 2011.

XS
SM
MD
LG